1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wasiwasi wakumba Bukavu DRC kufuatia tahadhari juu ya Ebola

Mitima Delachance, DW, Bukavu31 Julai 2019

Wasiwasi umezidi kukumba mji wa Bukavu kufuatia tahadhari juu ya mlipuko wa ugonjwa wa Ebola. Hakuna meli iliyoruhusiwa kutia nanga Jumatano kwenye bandari mbalimbali za Bukavu kuanzia asubuhi hadi saa tano mchana.

https://p.dw.com/p/3N5z3
Demokratische Republik Kongo l anhaltende Ebola-Epidemie
Picha: picture alliance/AP Photo/J. Delay

Nchini jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, hali ilikuwa ya wasiwasi mjini Bukavu tangu mapema asubuhi ya leo kufuatia tahadhari juu ya mwanamke ambaye huenda ni mtu wa pili  ambae ameambukizwa virusi vya Ebola ambapo mtu mmoja alithibitishwa kufariki mjini  Goma Jumanne iliyopita. Hakuna meli iliyoruhusiwa kutia nanga Jumatano kwenye bandari mbalimbali za Bukavu kuanzia asubuhi hadi saa tano mchana.

Tangu mapema asubui, boti kadhaa zilibaki ziki zunguka juu ya maji ya Ziwa Kivu, boti hizi ambazo zingepaswa kutia nanga ndani ya bandari hii saa kumi na mbili asubuhi, lakini zimezuiwa na agizo la Gavana Theo Ngwabidje ambaye alifafanua kwamba ni katika lengo la kukingia jimbo lake dhidi ya Ebola.

Abiria walibaki kwa hofu nyingi ndani ya boti hizo wakisubiri hadi saa tano wakati timu maalum zinazohusika na afya zilipo maliza kulitenga  eneo  hilo.

Operesheni ya kutoa chanjo dhidi ya Ebola kuanza katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Operesheni ya kutoa chanjo dhidi ya Ebola kuanza katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya CongoPicha: Reuters/O. Acland

Baadae timu hizo zili lazimisha kila biria kujitambulisha, mashua kwa mashua, huku zikichukua pia joto lao kwa njia ya vipimo vya joto kwenye chombo  maalum na kuamuru abiria waoshe mikono yao katika maji yaliyotiwa dawa.

Halafu wanatengwa kando kwa dakika chache ili kujihakikishia kwamba hakuna mtu aliyeponyoka, kabla ya kuwaruhusu kila mtu kwenda nyumbani kwake. Hatimaye boti hizo zote tano zimefanyiwa uchunguzi na hakuna kesi ya Ebola iliyopatikana. Hata hivyo, Gavana wa kivu kusini, Theo Ngwabidje ameonya wakaazi kuwa makini.

Mbali na kufahamu umuhimu wa kuzuiliwa huko, baadhi ya abiria waliokuwa ndani ya boti hizo wamelalamikia muda wao uliopotezwa bure wakati wa utafiti huo.

Asasi za kiraia mjini Bukavu zimechukua fursa hii na kuonya serikali ya mkoa wa Kivu Kusini kuweka timu za matibabu kwenye ziwa kivu ili kufanya uchunguzi zaidi kati ya miji ya Bukavu na Goma.