1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 18 wauawa katika shambulio Burkina Faso

Sylvia Mwehozi
14 Agosti 2017

Washambuliaji wanaosadikiwa kuwa wapiganaji wa Kiislamu wenye misimamo mikali wamevamia mgahawa mmoja wa Kituruki katika mji mkuu wa Burkina Faso, jana Jumapili na kuwaua watu wasiopungua 18.

https://p.dw.com/p/2iAVJ
Terroranschlag in Burkina Faso
Picha: Reuters

Hilo ni shambulio la pili la aina hiyo kwenye mgahawa maarufu ulio na idadi kubwa ya raia wa kigeni katika kipindi cha miaka miwili. 

Waziri wa mawasiliano wa Burkina Faso Remi Dandjinou amewaambia waandishi wa habari kwamba watu wasiopungua 18 wameuawa na wengine 8 kujeruhiwa huku washambuliaji wawili pia wakiuawa.

Amesema operesheni ya kukabiliana na washambuliaji hao imemalizika lakini msako mkali unaendelea katika mji wa Ouagadougou na vitongoji vya karibu.

Terroranschlag in Burkina Faso
Polisi wakikabiliana na washambuliaji mjini OuagadougouPicha: Reuters

Wahanga wa tukio hilo ni raia kutoka nchi tofauti, mmoja ametambulika kuwa ni raia wa Ufaransa. Nayo wizara ya mambo ya nje ya Uturuki imesema raia wake mmoja ni miongoni mwa waliouawa katika mkasa huo.

Hakuna kundi lililodai kuhusika na shambulio hilo lililoendelea hadi saa za asubuhi leo jumatatu. Milio ya risasi ilisikika masaa saba baada ya shambulio hilo kufanyika.

Vikosi vya usalama viliwasili kwenye eneo la tukio na magari yaliyojihami baada ya kupokea ripoti za milio ya risasi karibu na mgahawa wa Aziz Istanbul, ulioko katika mji wa Ouagadougou.

Kapteni wa polisi Guy Ye amesema washambuliaji watatu walifika katika mgahawa huo kwa pikipiki na kuanza kufyawatulia risasi hovyo umati uliokuwa ukijipatia chakula cha usiku.

Tayari ubalozi wa Ufaransa nchini humo unafanya mawasiliano na mamlaka za ndani kuhusiana na shambulio hilo huku ikiwashauri raia wake kuepuka eneo hilo, imesema wizara ya mambo ya nje ya Ufaransa.

Terroranschlag in Burkina Faso
Baadhi ya wateja wa mgahawa ulioshambuliwa wakikimbia kujinusuruPicha: Reuters

Mwanamke mmoja aliyeshuhudia na mteja wa mgahawa huo Aline Kabore anasimulia ilivyokuwa."Tulikuwa tumemaliza kula na tukaondoka, tulikuwa tukimsubiri dereva nje aje kutuchukua. Mara tukasikia risasi, baada ya hapo, sijaona chochote tena".

Burkina Faso taifa la Afrika Magharibi lisilo na njia ya bahari, ni mojawapo ya nchi maskini zaidi duniani, na inapakana na Mali upande wa Kaskazini ambayo imekuwa ikikabiliana na wanamgambo wa Kiislamu.

Washambuliaji watatu katika mauaji ya mwaka jana walikuwa na asili ya kigeni, kwa mujibu wa kundi la wanamgambo wa Kiislamu la al-Qaida katika Maghreb (AQIM), ambalo lilidai kuhusika katika matukio hayo kwa kushirikiana na kundi la wanajihadi linalojulikana kama al Mourabitoun.

Wataalamu wanasema kitisho cha ugaidi nchini Burkina Faso kinaendelea kuongezeka kwasababu ya ugaidi wa ndani.

Mpaka katika mkoa ulioko Kaskazini kwa hivi sasa ni nyumbani kwa mhubiri wa ndani Ibrahim Malam Dicko, ambaye amekuwa na itikadi kali na alidai kuhusika katika mashambulizi ya hivi karibuni dhidi ya vikosi vya usalama na raia. Taasisi yake ya Kiislamu ya Ansarul sasa inachukuliwa kama kundi la kigaidi na serikali ya Burkina Faso.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AP/Reuters

Mhariri: Iddi Ssessanga