1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 443 wafa katika mafuriko ya Afrika Kusini

19 Aprili 2022

Mvua kubwa inayonyesha Afrika Kusini imewaua karibu watu 443 na wengine kadhaa bado hawajulikani waliko. Mamlaka ilisema kuwa wanajeshi 10,000 wapo katika maeneo ya tukio ili kusaidia zoezi la uokoaji.

https://p.dw.com/p/4A6H9
Südafrika Überschwemmungen Regen
Picha: Rogan Ward/REUTERS

Rais wa nchi hiyo Cyril Ramaphosa ametangaza jana janga la kitaifa nchini humo. Kwenye hotuba yake ya televisheni, Rais Ramaphosa amesema karibu watu 48 hawajulikani waliko.Mvua kubwa iliukumba mkoa wa KwaZulu Natal tangu Aprili 11. Mvua hiyo imesababisha uharibifu mkubwa wa barabara, madaraja na nyumba na kutatiza usambazaji wa chakula na mafuta. Rais huyo amesema inakadariwa kwamba watu 40,000 wameachwa bila makaazi kutokana na mafuriko hayo. Bandari ya Durban ambayo ni mojawapo ya bandari kubwa zaidi za mizigo barani Afrika imefungwa na baadhi ya maeneo hayana umeme au maji safi ya kunywa. 

Südafrika Überschwemmungen Regen
Barabara iliyoharibika kwasababu ya mafuriko Picha: ROGAN WARD/REUTERS

Wiki moja baada ya dhoruba kali kuikumba pwani ya mashariki mwa Afrika Kusini, mamlaka ilisema siku ya Jumatatu kuwa wanajeshi 10,000 wapo katika maeneo ya tukio ili kusaidia zoezi la kuwatafuta watu 63 ambao hawajulikani walipo na pia kurejesha huduma muhimu.

Mamlaka ya jimbo la KwaZulu-Natal imesema mafuriko hayo ni moja ya majanga mabaya zaidi kuwahi kushuhudiwa katika historia ya Afrika Kusini. Wakati mazishi yakifanyika kote mjini Durban, ambako kumekumbwa na dhoruba hiyo, matukio ya kutisha ya janga hilo yameendelea kuibuka. Takriban watu 40,000 wameachwa bila makaazi na zaidi ya shule 550 na karibu vituo 60 vya huduma za afya vimeharibiwa. Serikali imetangaza kutolewa kwa dola milioni 68 kama msaada wa dharura.