1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waturuki wakasirishwa na Ujerumani

Yusra Buwayhid3 Juni 2016

Uturuki imekasirishwa na Ujerumani, kwa kuyatambua mauaji yaliyofanywa na utawala wa Ottoman dhidi ya Waarmenia mwaka 1915 kuwa ni ya halaiki. Mauwaji yalifanyika miaka 100 iliyopita, wakati wa vita vya kwanza vya dunia

https://p.dw.com/p/1IzoZ
Türkei Proteste gegen die Armenienresolution vor der deutschen Botschaft in Istanbul
Picha: Getty Images/AFP/O. Kose

Raia wa kawaida wana wasiwasi kwamba uamuzi huwo wa Ujerumani, utaharibu mahusiano kati ya nchi hizo mbili pamoja na kuchelewesha kutatuliwa kwa mgogoro wa wahamiaji.

Kitendo cha bunge la Ujerumani kupitisha azimio la kuyatambua mauaji hayo ya Waarmenia kuwa ni ya halaiki, kimezua upinzani mkubwa nchini Uturuki. Wanasiaa wa Kituruki wameukosoa vikali uamuzi huwo, hususan rais Recep Tayyip Erdogan, huku raia wa kawaida wakiwa na wasiwasi kwamba mahusiano kati ya nchi zao huenda yakaharibika.

Mamia ya Waturuki wameandamana nje ya ubalozi mdogo wa Ujerumani mjini Istanbul, kupinga uamuzi huwo wa bunge la Ujerumani.

"Hili ni suala la kujadiliwa miongoni mwa wanahistoria na sio suala la kujadiliwa na wanasiasa," amesema Rabia Gul, miongoni mwa wandaamanaji hawo.

Kutokana na hali ya chi ilivyo kwa sasa, kwa kuundwa serikali mpya hivi karibuni, kuongezeka kwa mapambano dhidi ya chama cha wafanyakazi cha Wakurdi (PKK) pamoja na uchumi wa nchi kukwama, uamuzi wa Ujerumani kuhusu mauaji ya kimbari ya Warmenia si suala la kuwapa wasiwasi Waturuki kwa sasa.

Lakini licha ya yote hayo wengi katika jamii ya watu wa Uturuki wanaunga mkono msimamo wa serikali, wa kukana kwamba mauaji hayo yanastahili kuitwa ya halaiki.

Hoja za raia wa Kituruki

Deutschland Debatte im Bundestag um Anerkennung des Völkermordes durch die Türkei an den Armeniern
Mjadala wa bunge la Ujerumani kuyatambua mauaji ya Waarmenia yaliyofanywa na Uturuki kuwa ni ya kimbariPicha: picture-alliance/dpa/Bildfunk/P. Zinken

DW imekusanya maoni ya umma juu ya uamuzi huwo mjini Istanbul, na kwa mujibu wa Ayfer Öztürk raia wa Uturuki, anasema uamuzi wa Ujerumani wa kuyatambua mauaji ya Waarmeni kama ni ya halaiki hauwasaidii kitu Warmenia wala Waturuki.

"Suala hili ilikuwa lishughulikiwe na wanahistoria. Lakini linaendelea kujadiliwa bungeni. Öztürk ameongeza kwamba mataifa ya Ulaya mara kwa mara yanalizusha suala hili la mauaji ya Waarmenia kama njia moja wapo ya kuishinikiza Uturuki," anahoji Öztürk.

Kwa upande mwengine kuna wale wanaoamini kwamba, bunge la Ujerumani kwa kuyataja mauaji hayo kuwa ya halaiki, litasababisha mvutano katika harakati za kusaidiana kuutatua mgogoro wa wakimbizi.

Mwalimu wa shule Sinan Arsel anasema uamuzi wa bunge la Ujerumnai haukuwa wa kisheria bali ni wa kisiasa. Arsel anasema kuibua tena janga lilofanyika miaka 100 iliyopita katika ajenda ya hivi sasa ni kinyume na maadili.

"Hata kama kujadili suala kama hili kunaendana na maadili ya nchi ya Ulaya. Kuibua tukio linaloweza kuchelewesha mchakato wa kupambana na mgogoro wa wahamiaji, ni makosa. Ndio maana ni tabu kuuheshimu uamuzi wa Ujerumani. Hatua hii kwa hakika, itaathiri ushirikiano unaotarajiwa kuwepo kati ya Ujerumani na Uturuki kutatua mzozo wa wahamiaji," anaeleza Arsel.

Mwandishi: Aram Ekin Duran, Istanbul

Tafsiri : Yusra Buwayhid

Mhariri: Hamidou Oummilkheir