1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wazimbabwe wajitayarisha kwa uchaguzi Jumatatu

Sekione Kitojo
29 Julai 2018

Katika treni yendayo taratibu usiku kutoka Johannesburg kwenda mpakani na Zimbabwe,mazungumzo ni iwapo uchaguzi kesho Jumatatu(30.07.2018)unaweza kuleta mshangao na kuiangusha serikali inayoongozwa na chama cha ZANU-PF.

https://p.dw.com/p/32Fwr
Simbabwe Wahlkampf Präsident Mnangagwa
Picha: Reuters/P. Bulawayo

Wasafiri  wa  kawaida  waliobeba  mahindi, mablanketi  na  sabuni za  kufulia walikaa pamoja  na  wapiga  kura  wakielekea  nyumbani kwa  ajili  ya  uchaguzi wa  kwanza  nchini  Zimbabwe  tangu kiongozi aliyeongoza  nchi  hiyo  kwa  mkono  wa  chuma Robert Mugabe kuondolewa  madarakani miezi  minane  iliyopita.

Zimbabwe, Nelson Chamisa
Mgombea wa upinzani wa chama cha MDC Nelson Chamisa(katikati)Picha: picture-alliance/T.Mukwazhi

Mabehewa  sita  ya  treni  hiyo iliondoka  katika  kituo  kikuu  cha mjini  Johannesburg  cha  Central Park mapema  jioni  ya  Ijumaa katika  safari  ya  masaa 15, ya  kilometa 600 katika  majira  haya ya  baridi.

"Watu wa Zimbabwe  wanahitaji  maisha  mapya  ili  waweze kusahau juu  ya maisha  magumu  tuliyopitia  chini ya  yule  mzee Mugabe," amesema  abiria  mmoja  Emile Manyikunike, mwenye umri  wa  miaka  36, akivalia  koti  la  baridi  la  ngozi lenye  rangi nyeusi na  fulana ya  kijani  yenye  picha  ya  Bob Marley.

"Watu walikuwa  wanapigwa na  polisi kwa  kutokubaliana  na serikali, na hata  hatukuweza  kuwaamini majirani  zetu  kwasababu kila  mtu  wa  pili  alikuwa  ni mpelelezi  wa  ZANU-PF," aliliambia shirika  la  habari  la  AFP.

Simbabwe Wahlen
Mojawapo ya mabango yanayohimiza upigaji kura kwa vyama vinavyoshiriki uchaguzi nchini ZimbabwePicha: DW/C. Mavhunga

Manyikunike amesema  anamuunga  mkono Nelson Chamisa, kiongozi  kijana  wa  chama  cha  upinzani  cha  MDC ambaye  ana matumaini  ya  kumshinda  mshirika  wa  zamani   na  mrithi  wa Mugabe, Emmerson Mnangagwa  wa  chama  cha  ZANU-PF.

Chini  ya  utawala  wa  mugabe , uchumi  wa  Zimbabwe uliporomoka  na  mamilioni  walikimbilia  nje  ya  nchi , hususan katika nchi  jirani  ya  Afrika  kusini kutafuta kazi na  kukimbia  utawala  huo wa kikandamizaji.

"Chamisa  anhitaji  kuhakikisha  kwamba  Wazimbabwe  wote wanapata  ajira ili kwamba  hata  wale  ambao  wanakimbia wanaweza  kurejea  na  kuijenga  nchi  yetu," manyikunike  aliliambia shirika  la  habari  la  AFP.

Wazimbabwe wana shauku ya kupiga kura

"Treni  hii  inanipeleka  nyumbani  ili niweze  kupiga  kura  na  kuleta mabadiliko."

Kofi Annan
Mmoja wa waangalizi wa uchaguzi wa Zimbabwe mara hii ni katibu mkuu wa zamani wa UN Koffi AnnanPicha: DW/P. Musvanhiri

Abiria  mwenzake  Gertrude Tshabalala, mwenye  umri  wa  miaka 58 , mfanyakazi  wa  nyumbani  nchini  Afrika  kusini, alikuwa anaelekea  nyumbani  kuwatembelea  wajuu  zake wanne, akiwa amebeba sufuria  za  kupikia, vyakula vya makopo  na  nyama  ili kuweza  kusaidia uhaba wa  vyakula  nchini  Zimbabwe.

Ana shaka  iwapo Mnangagwa  na  ZANU-PF , chama  ambacho kimeitawala  nchi  hiyo  tangu  kupata  uhuru  kutoka  Uingereza mwaka  1980, anaweza  kushindwa  katika  nchi  ambayo  imekuwa na historia  ya  udanganyifu  katika  uchaguzi.

"ZANU-PF hushinda  kila  mara , bila  kujali chochote," alisema . "Lakini  wajukuu  zangu  wawili  ni  wana umri  wa  kupiga  kura mwaka  huu  na natumai tu kwamba  kura  zao  zitaleta  tija  tofauti na  zetu  huko  nyuma."

Simbabwe Robert Mugabe 2017, Präsident
Kiongozi wa muda mrefu wa Zimbabwe Robert Mugabe aliondolewa madarakani miezi minane iliyopitaPicha: picture-alliance/AP Photo/B. Curtis

"Tunarudi  nyumbani  kwa  kuwa  tunataka  nchi  mpya. Ilikuwa  miaka 37 na  mzee  yule  akitawala , alikuba  bahili  na  alitaka  kila  kitu kwa  ajili  yake tu," alisema mhudumu  muuguzi, ambaye anafanyakazi  mjini  Johannesburg kwa  miaka  sita  sasa.

 

"Nakwenda  kumpigia  kura kijana  Chamisa. Wazee wanataka wazee  wenzao. Akili  zao  zimezeeka, hawawezi  kufikiri  vizuri."

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Lilian Mtono