Waziri Mkuu al-Maliki aimarisha uwezekano wa kubakia madarakani
15 Machi 2010Matoeko ya mwanzo yanaonyesha kuwa chama cha "State of Law Alliance" cha al-Maliki kinaongoza katika majimbo mawili kutoka majimbo matatu makubwa kabisa nchini humo. Chama hicho kipo mbele katika majimbo 7 kutoka jumla ya majimbo 18, lakini hizo si tarakimu za mwisho. Tarakimu za mwanzo zilizotolewa siku ya Jumapili zimeonyesha kuwa al-Maaliki alie wa madhehebu ya Kishia anaongoza kwa wingi mkubwa katika eneo la kusini la Basra lililo na utajiri wa mafuta na katika mji mtakatifu Karbala.
Muungano wa vyama vya Kishia, unaoongozwa na Waziri Mkuu al-Maliki, tayari ulikuwa ukiongoza katika mji mkuu Baghdad unaopeleka wajumbe 70 katika bunge lenye viti 325. Kundi hilo pia linashika nafasi ya mbele katika majimbo ya Babil, Najaf, Wasit na Muthanna yaliyo na Washia wengi zaidi. Hata hivyo, tarakimu hizo huenda zikabadilika, kwani ni matokeo ya asilimia 18 tu ya kura zilizohesabiwa. Maafisa wa Tume ya Uchaguzi wamesema, tarakimu mpya zitatolewa baadae leo hii.
Lakini vyama vya upinzani vinadai kuwa kumefanywa udanganyifu katika uchaguzi na hata wakati wa kuhesabiwa kura. Waziri Mkuu al-Maliki amepuuza malalamiko hayo na kusema kuwa kulikuwepo ila ndogo tu. Alipozungumza kwenye televisheni Jumapili usiku alisema, hayo ni malalamiko yasioweza kuathiri matokeo ya uchaguzi. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kuonekana hadharani tangu ofisi yake kutangaza Alhamisi iliyopita kuwa alifanyiwa operesheni katika hospitali moja mjini Baghdad, lakini hakujatolewa maelezo zaidi.
Hata maafisa wa tume ya uchaguzi wamepuuza tuhuma za udanganyifu. Faraj al-Haidari, anaeongoza tume hiyo, amewaambia waandishi wa habari, malalamiko ya safari hii ni nusu ya yale yaliyotolewa wakati wa uchaguzi wa serikali za mikoa uliyofanywa Januari iliyopita. Tume hiyo imewaomba wananchi kuwa na subira kwani matatizo yaliyotokea mara kwa mara katika mitambo ya compyuta yamechelewesha kutoa matokeo ya uchaguzi.
Wakati huo huo, hesabu zilizotolewa jana zimeonyesha kuwa waziri mkuu wa zamani, Iyad Allawi, ambae ni wa madhehebu ya Kishia kama al- Maliki anaongoza katika jimbo la kaskazini la Kirkuk, kinyume na vile ilivyotabiriwa kuwa ushindi utanyukuliwa na kundi la Wakurdi linalotaka kuliingiza eneo hilo lenye utajiri wa mafuta katika jimbo lao la kaskazini lililo na utawala wa ndani. Allawi pia anapiga fora katika jimbo la Anbar lililokuwa likidhibitiwa na Waarabu wa madhehebu ya Kisunni.
Matokeo kamili ya uchaguzi yanatazamiwa kutangazwa tarehe 18 mwezi huu wa Machi na hesabu za mwisho kabisa huenda zikatolewa mwishoni mwa mwezi baada ya malalamiko yote kuchunguzwa.
Mwandishi: Martin,Prema/AFPE
Mhariri: Othman,Miraji