1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri Mkuu wa Sudan Hamdok awasili Juba

Amina Mjahid
12 Septemba 2019

Waziri Mkuu mpya wa Sudan Abdalla Hamdok amewasili Sudan Kusini kwa ziara yake ya kwanza rasmi tangu kuchukua wadhifa wake, akiahidi uhusiano usio na mipaka kati ya maadui hao wa zamani.

https://p.dw.com/p/3PUlq
Sudan Neuer Premierminister Abdalla Hamdok
Picha: Reuters/M. Nureldin Abdallah

Hamdok, anayeongoza serikali ya mpito iliyo ya mawaziri 18 kufuatia kuondolewa rais wa muda mrefu nchini humo Omar al Bashir, anatarajiwa kukutana na rais wa Sudan Kusini Salva Kiir pamoja na viongozi wa upinzani wa Sudan katika ziara yake hiyo ya siku mbili.

" Nafurahi kufika hapa katika nchi yangu ya pili  tunatafuta mkakati mzuri wa mahusiano kati ya nchi zetu na tutafanya kila liwezekanalo kufanikisha hilo," alisema Hamdok alipowasili Sudan Kusini.

Waziri Mkuu huyo mpya wa Sudan Abdalla Hamdok amesema anataraji mahusiano ya mataifa hayo mawili yatakuwa ya mafanikio, yatakayojadili masuala ya biashara mipaka, mafuta, na utembeaji huru wa watu katika mataifa hayo.

Sudan Kusini ilijitenga kutoka eneo la Kaskazini mwaka 2011 baada ya miongo kadhaa ya mapigano mjini Khartoum na kuwa taifa changa duniani na miaka miwili baadae ikatumbukia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Je Hamdook anaweza kweli kumpatanisha Salva Kiir na Riek Machar

Südsudan -  Riek Machar und  Salva Kiir
Makamu wa rais wa zamani wa Sudan Kusini Riek Machar na rais wa nchi hiyo Salva KiirPicha: Reuters/M. N. Abdallah

Lakini huku hali ya wasiwasi ikiendelea kutanda kati ya Sudan na upande wa Kaskazini kuhusiana na mgogoro wa mpakani na usafirishaji wa mafuta kwenda Kaskazini, mataifa hayo mawili yamechukua hatua za kujaribu kurejesha uhusiano mzuri kati yao katika miaka ya hivi karibuni.

Kwa upande wao wachambuzi wanasema mataifa hayo mawili yamelazimika kuwa na mahusiano mazuri kufuatia vita vya Sudan Kusini, vilivyokiuka makubaliano kadhaa ya kusimamisha vita hivyo na mgogoro wa kisiasa uliyoikumba Sudan uliyoathirika vibaya baada ya kuporomoka kwa sekta yake ya mafuta.

Hatua ya mwisho ya rais wa zamani Omar al Bashir kabla ya kuondolewa madarakani ni kujaribu kupata makubaliano ya amani kati ya rais Salva Kiir na hasimu wake Riek Machar wakati ambapo baadhi ya mataifa duniani yalishindwa  kupata suluhu ya kuutatua mgogoro huo.

Hata hivyo mpango wa amani wa mwaka 2018 ulikwama kufuatia Sudan nayo kutafuta njia ya kukabiliana na mgogoro wa kisiasa. Wachambuzi kwa sasa wanafuatilia kuona iwapo serikali mpya ya Sudan  itaweza kumshawishi Kiir na Machar kuingia tena katika mazungumzo ya amani.

Wawili hao walikutanamjini Juba hivi karibuni baada ya miezi mitano huku serikali ya kugawana madaraka ikitarajiwa kuundwa ifikapo mwezi Novembamwaka huu.

Chanzo: Mashirika