1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tsipras awafuta kazi waasi chamani

18 Julai 2015

Waziri mkuu wa Ugiriki Alexis Tsipras jana Ijumaa (17.07.2015)amewafuta kazi mawaziri ambao wameasi kuhusiana na masharti magumu ya uokozi wa uchumi wa nchi hiyoyaliyokubaliwa wiki hii.

https://p.dw.com/p/1G0sM
Belgien Euro-Gipfel erzielt Einigung bei Griechenland
Waziri mkuu wa Ugiriki Alexis TsiprasPicha: Reuters/E. Vidal

Hatua hiyo inaelekeza katika kuuweka uchumi wa nchi hiyo katika hali bora kabla ya duru mpya ya majadiliano magumu pamoja na wakopeshaji ikiwa ni pamoja na Ujerumani, ambayo imeidhinisha makubaliano hayo.

Mhanga maarufu wa hatua hiyo ya Tsipras ni waziri wa nishati Panagiotis Lafazanis, mkuu wa kikundi cha wenye msimamo mkali ndani ya chama cha waziri mkuu Tsipras, kikundi ambacho kimedai nchi hiyo ijitoe kutoka katika kanda ya sarafu ya euro. Mshirika wake, naibu waziri wa ulinzi pia ameondolewa.

Mabadiliko hayo ya baraza la mawaziri yamekuja saa chache tu baada ya Umoja wa Ulaya kuidhinisha kiasi cha euro bilioni 7.16 ikiwa ni mkopo wa dharura kwa Ugiriki, utakaoiwezesha kulipa fedha nyingi kuanzia mapema wiki ijayo kwa wakopeshaji wake. Wakati huo huo, mpango mpya wa nchi za ukanda wa sarafu ya euro wa kuuokoa uchumi wa Ugiriki ukijadiliwa.

Griechenland Energie- und Umweltminister Panagiotis Lafazanis
Waziri wa nishati na mazingira Panagiotis Lafazanis aliyefutwa kaziPicha: Reuters/A. Konstantinidis

Pia inafuatia hatua ya wabunge wa Ujerumani kumpa Kansela Angela Merkel idhini ya kuanza majadiliano kuhusiana na mpango mpya wenye thamani ya euro bilioni 86.

Waziri mkuu wa Ugiriki akitiwa hamasa na matumaini mapya ya msukumo mpya kwa ajili ya mazungumzo baada ya kukandamiza uasi wa wabunge katika chama chake cha siasa kali za mrengo wa shoto cha Syriza hali iliyoidhoofisha serikali na kuleta hofu ya kufanyika kwa uchaguzi wa mapema.

Mabadiliko hayo ya serikali, ambayo yameshuhudia mabadiliko tisa, yamewakumba manaibu mawaziri wa fedha na mambo ya kigeni, ambao wamejiuzulu kuhusiana na mpango huo. Wajumbe wapya wa baraza la mawaziri wanatarajiwa kuapishwa katika sherehe itakayofanyika hii leo Jumamosi(18.07.2015).

Merkel ambaye kama Tsipras anakabiliwa na uasi katika chama chake, amewaambia wabunge nchini Ujerumani kwamba makubaliano na Ugiriki ilikuwa ni nafasi ya mwisho kuzuwia ghasia katika nchi hiyo iliyokumbwa na mzozo.

Deutschland Bundestag Sondersitzung Griechenland
Kansela wa Ujerumani Angela MerkelPicha: Getty Images/AFP/T. Schwarz

Mwishowe alifanikiwa kupata uungwaji mkono mkubwa kwa kuidhinishwa na bunge la nchi hiyo Bundestag, ambapo muungano wake unaounda serikali una wingi mkubwa wa wabunge, ambapo wabunge 439 walipiga kura ya ndio, 119 walipinga na 40 hawakupiga kura.

Akihutubia bunge kabla ya kupiga kura , Merkel alidai kuwa "tutakuwa uzembe kwa kiasi kikubwa, na kutowajibika, iwapo hatutajaribu njia hii".

Ni Merkel, kiongozi wa nchi yenye uchumi mkubwa katika Umoja wa Ulaya na mchangiaji mkubwa katika mpango huo wa uokozi, ambaye ameongoza mbio za wiki iliyopita za mazungumzo mjini Brussels ambayo yameiondoa Ugiriki ukingoni mwa kutupwa nje ya ukanda wa sarafu ya euro.

Mwandishi: Sekione Kitojo / afpe

Mhariri: Caro Robi