1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa Nje wa Ujerumani ziarani Marekani

N.Buschschlüter - (P.Martin)3 Februari 2009

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier leo anakutana na waziri mwenzake wa Marekani Hillary Clinton mjini Washington.

https://p.dw.com/p/Gm8k
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier.

Steinmeier hasa angependa kupata sura kamili ya sera za nje za serikali mpya ya Marekani.Yeye anataka kujiarifu juu ya sera muhimu za nje za Marekani kwani kwa maoni yake ajenda ya kimataifa inahitaji uratibu wa haraka kutoka Marekani na Ulaya.Kuna mada nyingi za kujadiliwa:lakini mada itakayopewa kipaumbele katika mkutano wa kwanza wa Clinton na Steinmeier bila shaka ni Iran na Afghanistan.

Serikali mpya ya Marekani iliposhika madaraka ilisema,Afghanistan ipo katika mstari wa mbele kupiga vita ugaidi na inatazamia kupeleka wanajeshi 30,000 ziada katika kipindi cha miezi 18 ijayo.Marekani inataka msaada zaidi nchini Afghanistan kutoka washirika wake.Mkutano wa mawaziri hao wawili unafanywa siku moja kabla ya mkutano wa nchi tano wanachama wa kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa yaani Marekani, Uingereza,Ufaransa,Urusi na China pamoja na Ujerumani pia.Wajumbe wa nchi hizo watakutana Jumatano mjini Berlin kujadili suala la nyuklia pamoja na Iran.

Mada zingine zitakazojadiliwa hii leo mjini Washington ni mzozo wa kiuchumi unaoathiri dunia nzima, mabadiliko ya hali ya hewa duniani, usalama wa nishati na mkutano wa kilele wa NATO utakaofanywa mwezi Aprili.Kwa mujibu wa duru za ujumbe unaofuatana na Steinmeier,waziri huyo atakapokutana na Clinton ataitumia fursa hiyo pia kusaidia kupunguza hali ya mvutano katika uhusiano wa Marekani na Urusi.Kwani katika suala la kuzuia usambazaji wa silaha,waziri wa nje wa Ujerumani amesema kuwa ameona msimamo mpya.Kwa maoni yake,mada kama hiyo ghafla ni rahisi kujadiliwa na serikali mpya ya Marekani. Amesema,tangu ziara ya kwanza ya Obama mjini Berlin ilikuwa hivyo na hata wakati wa mazungumzo yake ya kwanza ya simu na Waziri wa Nje wa Marekani ilikuwa hivyo hivyo

Suala jingine linalotazamiwa kujadiliwa ni iwapo Ujerumani itakubali kuwachukua wafungwa watakaoachiliwa kutoka jela ya kijeshi ya Marekani ya Guantanamo Bay kisiwani Kuba.Marekani inayotazamia kuifunga jela hiyo mwishoni mwa mwaka huu,haikupeleka ombi rasmi kwa serikali ya Ujerumani.Hata hivyo Berlin imetengana kuhusu suala hilo.Haijulikani iwapo Waziri wa Nje wa Ujerumani atakutana na Rais wa Marekani Barack Obama wakati wa ziara hiyo fupi mjini Washington.Viongozi hao wawili walikutana kwa mara ya kwanza Julai mwaka jana pale Obama alipolitembelea jiji la Berlin kama mgombea urais.