1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa zamani wa Rwanda atiwa nguvuni Ujerumani

Mohammed AbdulRahman20 Septemba 2007

Baada ya zaidi ya muongo mmoja tangu mauaji hayo yalipotokea nchini Rwanda , hatimae polisi nchini Ujerumani imemtia nguvuni mtuhumiwa mmoja wapo anayesakwa na mahakama ya kimatifa, ya Rwanda Waziri wa zamani Augustin Ngirabatware

https://p.dw.com/p/CH80
Makaburi ya wahanga wa mauaji ya halaiki ya 1994.
Makaburi ya wahanga wa mauaji ya halaiki ya 1994.Picha: AP

Bw Ngirabatware ambaye ni Mhutu na aliyekua Waziri wa mipango katika utawala huo wa zamani alitiwa nguvuni Frankfurt am Main. Mwanasheria mkuu wa Shirikisho mjini Frankfurt pamoja na ofisi ya shirikisho inayohusika na uhalifu wamethibitisha kukamatwa kwake. Kwa mujibu wa maafisa wa Ujerumani, Ngaribatware amekua akihama hama akiishi katika sehemu na hoteli tafauti Anasemekana aliwapa silaha wanamgambo wa kihutu wakati wa mauaji dhidi ya Watutsi na wahutu waliokua na msimamo wa wastani

Hatua ya kumtia nguvuni waziri huyo wa zamani, imepongezwa na waziri wa sheria wa Rwanda Tharcisse Karugarama na kuelezea matumaini yake kwamba zitachukuliwa hatua za haraka kumkabidhi kwa mahakama ya kimataifa kuhusu Rwanda yenye makao yake makuu katika mji wa kaskazini mwa Tanzania-Arusha. Akizungumza na Redio Deutsche welle kuhusu hatua ya Ujerumani kumtia nguvuni Bw Ngaribatware, muakilishi wa Rwanda katika mahakama hiyo ya Arusha Balozi Alois Mutabingwa pia aliipongeza Ujerumani kwa hatua hiyo na kusema ana matumaini nchi nyengine ambako kuna washukiwa kama hao zitachukua hatua za dhati kuhakikisha wahalifu wa aina hiyo wanafikishwa mbele ya sheria

Mtuhumiwa Ngirabatware myenye umri wa miaka 50, na aliyekua waziri wa mipango kuanzia 1990 hadi 1994 wakati wa utawala wa Juvenal Habiyarimana, alikimbia baada ya utawala huo kuanguka na aliishi kwanza nchini Gabon na badae Ufaransa. Mahakama ya Arusha anamtaka kujibu mashitaka ya kuhusika na mauaji ya halaiki nchini Rwanda. Hadi sasa mahakama hiyo imeshawakuta na hatia washtakiwa 28 na watano wengine kuachiwa huru . Mwaka jana alichapisha kitabu akiitaja mahakama hiyo ya kimataifa kuwa si halali.