1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Winnie Mandela afanyiwa mazishi ya kitaifa

Caro Robi
14 Aprili 2018

Maelfu ya watu wamekusanyika Jumamosi (14.04.2018) katika uwanja wa mpira wa Soweto kutoa heshima zao za mwisho kwa mwanaharakati wa kupinga ubaguzi wa rangi nchini Afrika Kusini Winnie Madikizela-Mandela.

https://p.dw.com/p/2w3LK
Südafrika Bebgräbnis von Winnie Madikizela-Mandela in Johannesburg
Picha: Reuters/S. Sibeko

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa ametoa heshima yake iliyojawa hisia akiahidi kupendekeza Bi. Winnie apokee heshima ya juu ndani ya chama tawala cha African National Congress ANC. Ramaphosa amemtaja Winnie kama mtu aliyekuwa akijivunia, mtetezi na mwenye kueleza kwa ufasaha aliyefichua uongo wa wabaguzi.

Amesema kuwekwa kizuizini, mateso na miaka ya marufuku ambayo Madikizela-Mandela alipitia, vilimtia hamasa kama mwanaharakati wa kisiasa, lakini pia vilisababisha majeraha makubwa ambayo hayajawahi kupona na kwa kiasi kikubwa kupuuzwa na rika nyingi.

Winnie Madikizela-Mandela aliyefariki Aprili 2, akiwa na umri wa miaka 81 amezikwa kwa heshima ya kitaifa ambapo jeneza lake lilibebwa na askari wakati mwili wake ukiingizwa katika uwanja wa Soweto.

Viongozi kadhaa wa nchi walihudhuria mazishi hayo akiwemo rais wa Congo Brazzaville Denis Sassou Nguesso, waziri mkuu wa taifa jirani la Lesotho Pakalitha Mosisili; na wajumbe wengine kutoka serikali za afrika na vyama vya ukombozi. Marais wa zamani wa Afrika Kusini Jacob Zuma na Thabo Mbeki pia nao walihudhuria mazishi ya mpambanaji huyo aliyejulikana mama wa taifa au mama Winnie.

Mwandishi: Caro Robi/Ap

Mhariri: Sylvia Mwehozi