1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zambia yapigwa kumbo AFCON 2013

Josephat Nyiro Charo30 Januari 2013

Timu ya kandanda ya taifa ya Zambia, Chipolopolo, imekuwa mabingwa watetezi wa kwanza kupigwa kumbo kwenye michuano ya kuwania kombe la mataifa ya Afrika kwenye mechi za makundi katika kipindi cha miaka 21 iliyopita.

https://p.dw.com/p/17TrG
Zambia's captain Christopher Katongo, left, and teammates celebrate after winning the African Cup of Nations final soccer match against Ivory Coast at the Stade de l'Amitie in Libreville, Gabon, Sunday Feb. 12, 2012. (Foto:Themba Hadebe/AP/dapd)
Africa Cup SambiaPicha: AP

Zambia ilitoka sare tasa jana dhidi ya Burkina Faso, ambayo imefuzu kuingia robo fainali ya mashindano ya mwaka huu, AFCON 2013, kwenye mechi iliyochezwa katika uwanja wa Mbombela nchini Afrika Kusini. Sare ya tatu kwa Chipolopolo haikutosha kuiwezesha kusonga mbele katika mashindano hayo.

Timu ya mwisho iliyoshinda kombe la mataifa ya Afrika na kushindwa kusonga mbele katika duru ya pili kwenye mashindano yaliyofuata ni Algeria mnamo mwaka 1992.

Fußballspieler aus Burkina Faso. Datum: 28.01.13 Copyright: DW/Haimanot Turuneh
Wachezaji wa Burkina FasoPicha: DW/H. Turuneh

Burkina Faso imeongoza katika kundi C na kuweka historia yake, huku ikifuzu kwa raundi ya pili kwa mara ya kwanza katika nchi ya kigeni. Burkina Faso imewahi kusonga mbele katika mashindano ya kuwania kombe la mataifa Afrika, mara moja tu wakati ilipoyaandaa mnamo mwaka 1998.

Kocha wa Burkina Faso, raia wa Ubelgiji, Paul Put, amesema anadhani huu ni ufanisi mkubwa kabisa wa timu ya nchi hiyo kwa kuwa iliwahi kuyaandaa mashindano hayo mara moja na ikafaulu kufika nusu fainali. "Lengo letu la kwanza tulitaka kufanya vyema zaidi kuliko mashindano ya hivi karibuni ya kombe la mataifa ya Afrika na tulikuwa tumefanikiwa kwa kutoka sare dhidi ya Nigeria na Ethiopia. Nadhani ni historia kwa Burkina Faso," akaongeza kusema kocha Put.

Zambia haikung'ara

Kocha wa Zambia, Herve Renard, amebakia kuwa mwingi wa matumaini na mwanafalsafa. "Ni bora uwe umeshinda kitu katika maisha yako, kuliko kuingia robo fainali kila mara lakini usifaulu kushinda chochote," amesema kocha huyo na kuongeza kusema, "Huu sio mwisho wa dunia. Zamani tulikuwa tukirudi nyumbani mara nyingi baada ya raundi ya kwanza, na leo lazima tukubali kwamba huu ni mchezo wa soka."

epa03103510 Herve Renard, coach of Zambia celebrates after his team won the Africa Cup of Nations Final between Zambia and Ivory Coast in Libreville, Gabon, 12 February 2012. EPA/STR EDITORIAL USE ONLY
Kocha wa Zambia, Herve RenardPicha: picture-alliance/dpa

Zambia haikuonyesha mchezo mzuri na mshambuliaji wake matata, Collins Mbesuma, alikosa nafasi kadhaa za kuutikisa wavu wa Burkina Faso. Kwa upande wao Burkina Faso walifahamu walihitaji sare tu kuweza kufuzu na waliridhika kucheza katikati mwa uwanja ili kupunguza kasi ya mchezo huo, hususan baada ya kumpoteza kipa wao mahiri, Alain Traore, kutokana na jeraha alilolipata dakika ya 10 ya mtanange huo.

"Viungo vya leo ilikuwa ni pilipili nyingi na chumvi kidogo kwenye mchuzi," ndivyo alivyotamka kocha wa Burkina Faso, Paul Put.

Zambia ilipata changamoto kubwa kutokana na hali ya uwanja wa Mbombela kuwa na mchanga mwingi. Kocha wa Chipolopolo, Renard, amesema, "Nikiulaumu uwanja basi watu watasema nalia, lakini nadhani baada ya mkutano huu na waandishi wa habari unahitaji tu kwenda uwanjani na ujionee kama inawezekana kucheza kandanda safi."

Nigeria yaitwanga Ethiopia

Kwenye mechi nyengine ya kundi C, Nigeria iliinyoa Ethiopia bila maji kwa kuitandika mabao 2-0 katika uwanja wa mjini Rustenburg. Kocha wa Nigeria, Stephen Keshi, amesema, "Ushindi huu ni wa Wanigeria wote popote walipo ulimwenguni. Huu ni wakati wa kushangilia."

Nigeria's attacker Victor Anichebe (C) struggles for possession of ball with Ethiopian skipper Samson Gebreegziabher (R) and Abebaw Bune during the African Cup of Nations qualifying match between the two countries in Abuja Sunday, March 27, 2011. Nigeria defeated Ethiopia 4 - 0. AFP PHOTO/PIUS UTOMI EKPEI (Photo credit should read PIUS UTOMI EKPEI/AFP/Getty Images)
Ethiopia ikichuana na NigeriaPicha: Getty Images/AFP

Ushindi wa Nigeria dhidi ya Ethiopia umewatia tumbo joto wachezaji huku wakisubiri kuvaana na Cote d'Ivoire kwenye robo fainali. Burkina Faso inasubiri kukwaana na mshindi wa mechi ya kundi C kati ya Togo na Tunisia mjini Nelsprut itakayochezwa baadaye leo. Ethiopia na Zambia wanafunganya virago na kuelekea uwanja wa ndege tayari kurejea nyumbani.

Mwandishi: Josephat Charo/APE/AFPE

Mhariri: Hamidou, Ummilkheir