1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ZANU PF na MDC mkutanoni 'Sauzi'

Kalyango Siraj25 Novemba 2008

Pande zinazohusika na mgogoro nchini Zimbabwe zinakutana tena nchini Afrika Kusini kwa duru nyingine ya mazungumzo yenye lengo la kuupatia ufumbuzi mkwamo wa kisiasa ambao umeathiri taifa hilo.

https://p.dw.com/p/G1pK
Thabo Mbeki,kushoto mpatanishi mkuu wa mgogoro wa Zimbabwe.Kulia ni rais MugabePicha: dpa - Bildfunk

Hata hivyo upande wa upinzani umeapa kuwa hautakubali hatua yoyote ya kuachwa nyuma katika mchakato wa kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na chama kinachoongozwa na rais Robert Mugabe.

Mkutano wa Afrika ya Kusini unayawakutanisha wajumbe kutoka vyama vikuu viwili husika.Chama cha ZANU PF cha rais Robert Mugabe,cha Movement for Democratic Change MDC cha Morgen Tsvangirai pamoja na MDC ya Arthur Mutambara.

Baado haijulikani ikiwa chama cha MDC cha Tsvangirai kinahudhuria mazungumzo hayo baada ya kutishia hapo awali kuyasusia kikidai kuwa ajenda ya mkutano inafaa ipanuliwe ili kuyahusisha masuala yote mengine muhimu.

Haikujulikana ni masuala gani hayo kinachotaka yajumulishwa ama ikiwa yamejumulishwa. Kiongozi wao alikutana na wajumbe wake jumatatu asubuhi mjini Johannesburg kujadili msimamo wao huo.

Kiini cha mkutano huo ni kubadili katiba ya nchi ili kuweka kifungu kinachokubali kugawana madaraka pamoja na kuliwezesha bunge la taifa kukubali nafasi ya waziri mkuu kuchukuliwa na kiongozi wa upinzani.

Rais wa Zimbabwe Robert Mugabe, pamoja na viongozi wa upinzani walitia sahihi makubaliano ya kugawana madaraka mwezi septemba mwaka huu.Lakini sintofahamu kuhusu chama gani kidhibiti wizara nyeti zimedumaza kwa kipindi cha zaidi ya miezi miwili juhudi za kuunda serikali hiyo ya umoja wa kitaifa.

Makundi husika na mgogoro huo yanazidi kushinikizwa kufikia muafaka kutokana na kuongezeka kwa mgogoro wa kibinadamu.Viongozi wa kikanda nao wanazidi kuingiwa na wasiwasi kutokan na habari za kulipuka kwa ugonjwa wa kipindupindu.

Takriban watu 300 na ushei wamekufa kutokan na ugonjwa huo,na maafisa wa shirika la afya la umoja wa mataifa wanasema kuwa ugonjwa huo umeenea karibu katika nusu ya nchi hiyo na kuhofia kuwa huenda ukusambaa katika maeneo mengine.

Afisa mmoja amesema kuwa tangu mwisho wa mwezi wa Agosti hadi Novemba 20 watu zaidi ya elf 7 wameambukizwa na wengine kuambukizwa katika wiki chache zilizopita.

Na hayo yakiarifiwa vyombo vya habari nchini Zimbabwe vinawashutumu wanachama wa kundi la wazee kwa kile vilichodai kuwa njama za kutaka kuiangusha serikali ilioko madarakani.Msemaji wa chama cha Mugabe cha ZANU PF Chistopher Mutswanga,

mwishoni mwa juma alikiambia kituo kimoja cha Televisheni serikali yake ilikuwa inachunguza kwa kina hao wazee ni akina nani na wanawakilisha nani,akisema kuwa kundi hilo si la kimataifa ambalo liko chini ya sheria za Umoja wa mataifa.

Wazee hao mkiwemo rais wa zamani wa Marekani Jimmy Carter na katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Koffi Annan pamoja na mke wa Mzee Nelson mandela Graca Machel walinyimwa visa kuingia Zimbabwe kufanya ziara ya kibinadamu,serikali ilidai kuwa safari yao haikuwa muhimu.

Gazeti la serikali ya Zimbabwe la The Herald limedai kuwa kundi la wazee ni sehemu ya mpango kabambe wa Marekani na Uingereza wa kutaka kuupindua utawala wa Mugabe.