1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zanzibar yapiga marufuku mapambo ya pesa kwenye sherehe

9 Aprili 2019

Serikali ya Zanzibar imepiga marufuku matumizi ya fedha za noti kwenye mapambo ya harusi na sherehe nyingine. Ni baada ya kuibuka taarifa juu ya kikundi kinachotengeneza fedha bandia.

https://p.dw.com/p/3GW2u
Tansania Budget
Picha: DW/Kizito Makoye Shigela

Maafisa waandamizi kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BOT) na Mkuu wa Mkoa wa Mjini magharib Ayoub Mohammed Mahmoud wamesema ni marufuku kutengeza pesa bandia, na kuwa ni lazima kila Mtanzania athamini pesa za nchi kwa kuzingatia matumizi sahihi kwa sababu ni tunu ya taifa.

Pamoja na kuwa baadhi ya watu wasio waaminifu hutengeneza fedha bandia na kuzisambaza kwa matumizi, lakini kumeibuka tabia nyengine hivi karibuni ya kutumia fedha hizo za noti kama mapambano kwa kushonea nguo, makoti, kanga, na kuzigandisha kwenye meza jambo ambalo limeonekana kama ni kushindana na kuoneshana.

Kwa mujibu wa Kanuni za adhabu sura 16 kifungu 332A, mtu yeyote, bila mamlaka, kwa kunuwia anaeharibu, anaechana, anaekata au vinginevyo anaechanachana noti yoyote ya benki au fedha ambayo inatumika kihalali, atakuwa anatenda kosa  na atakuhumiwa kutoa faini ya shilingi elfu tano kwa kila noti iliyoharibiwa au, akishindwa adhabu ya kifungo cha mwaka moja.

Hiyo ni sheria ya Tanzania Bara lakini kwa upande wa Zanzibar sheria namba 6 ya mwaka 2018 ya kanuni za adhabu kifungu 364, yenye kipengele A na B ambapo inasomeka kama ilivyo sheria ya Tanzania bara lakini kipengele B kimekwenda mbali zaidi na kinagusa noti na sarafu ambapo ni kosa kuivunja, kuiyeyesha au kuibandika alama au kuiwekea jina au maneno au alama, au kuitumia vyenginevyo na adhabu yake ni kifungo cha miaka miwili au faini isiozidi milioni mbili.

Kutokana na kuonekana bado matumizi sahihi ya fedha haajajulikana Benki Kuu kutoa imeanza kufundisha juu ya matumizi sahihi ya Fedha kwa maafisa wa serikali na wananchi wa ngazi mbali mbali.

 

Mwandishi: Salma Said