1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zimesalia saa chache kabla ya Barack Hussein Obama kuapishwa kua rais wa 44 wa Marekani

Oumilkher Hamidou20 Januari 2009

Ndoto ya Martin Luther King yageuka kua ukweli wa mambo nchini Marekani,rais wa kwanza mwenye asili ya kiafrika akabidhiwa madaraka

https://p.dw.com/p/Gcog
Rais mpya wa Marekani Barack Hussein Obama na mkewe Michelle wakiwa njiani kwenda kanisaniPicha: AP


Jiji la Washington linajiandaa kwa sherehe za kuapishwa rais mpya Barack Obama, muda wa masaa mawili kutoka sasa.Wakuu wa mji mkuu huo wa Marekani wanategemea wageni zaidi ya milioni mbili-idadi kubwa kabisa kuwahi kushuhudiwa hapo awali katika sherehe yoyote ile ya kuapishwa rais wa Marekani.


Saa zinaendelea kuhesabiwa kuanzia sasa hadi furaha na shangwe zitakapofikia kilele chake.Mamilioni ya watu wanatarajiwa kushuhudia kwa macho yao pale Barack Hussein Obama atakapopanda ngazi za jengo la bunge la Marekani-Kapitol,kulitosa gwaride la kijeshi litakalouzunguka mji mkuu wa Marekani na hatimae kuingia katika ikulu ya Marekani White House.


Mabasi elfu kadhaa yameanza kuingia Washington kutoka kila pembe ya Marekani na kuwapeleka hadi katika uwanja mkubwa wa mashabiki ambako burudani kubwa kabisa kuwahi kushuhudiwa katika mji mkuu huo itafanyika.Wanajesahi na polisi 40 elfu wanasimamia usalama,bila ya kusahau helikopta zinazopiga doria angani.



Kabla ya kuapishwa, rais mteule Barack Obama na makamu wake Joe Biden watahudhuria misa katika kanisa la St.John,karibu na ikulu ya Marekani.


Makamo wa rais Joe Biden ndie atakayeapishwa mwanzo kabla ya Barack Hussein Obama kuweka mkono wake juu ya biblia,ile ile iliotumika kumuapisha Abraham Lincoln mnamo mwaka 1861.Walimwengu wanasubiri kwa hamu kusikiliza hotuba itakayotolewa na rais huyo wa 44 wa Marekani,wa kwanza mwenye asili ya kiafrika.


Mshindi wa zawadi ya amani ya Nobel bibi Wangari Maathai amezungumzia matumaini ya Afrika na ulimwengu kwa jumla akionya dhidi ya kutegemea misaada kutoka Marekani.


Vijana pia wanajiwekea matumaini kumuona Barack Obama akileta mageuzi na amani ulimwenguni:



Na Mwenyewe Barack Obama anasema


"Nnapojiandaa kubeba dhamana ya rais,sauti zenu ndizo nitakazozikiliza kila wakati nitakapokua nikifanya kazi katika ofisi ya rais-oval office."


Sherehe za leo zitakamilika kwa densi ambapo rais Barack Hussein Obama na mkewe Michelle watashiriki katika densi tafauti zisizopungua kumi.