1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zuma adai kumuunga mkono Gordhan

Daniel Gakuba
25 Oktoba 2016

Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini amesema anamuunga mkono Waziri wa Fedha, Pravin Gordhan, ambaye wiki ijayo atasimama kizimbani kujibu shutuma za uhalifu ambazo zinaonekana kuwa na misingi ya kisiasa.

https://p.dw.com/p/2RguX
Südafrika Präsident Jacob Zuma
Picha: Imago/Gallo Images

Gordhan ambaye ni mwanachama mkongwe wa chama tawala ANC na anayeheshimiwa na wengi, anakabiliwa na shutuma zinazohusiana na malipo ya uzeeni kwa rafiki yake aliyestaafu.

Wachambuzi wengi wanashuku anaandamwa na washirika wa Rais Zuma katika mvutano unaoshamiri ndani ya chama cha ANC.

Zuma amesema baraza zima la mawaziri linasimama pamoja na Waziri Gordhan, ambaye amesema hana hatia hadi pale itakapotajwa vinginevyo na mahakama.

Gordhan amekuwa akipaza sauti yake dhidi ya ubadhirifu, na ufujaji wa fedha unaofanywa na serikali inayoongozwa na Rais Zuma.

Anaungwa mkono pia na Makamu Rais Cyril Ramaphosa, mawaziri kadhaa na viongozi wengi wa makampuni.