1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ASADABAD: Mwandishi wa habari Mjerumani aachiliwa huru

25 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBfJ

Mwandishi wa habari raia wa Ujerumani aliyeripotiwa kutekwa nyara mashariki mwa Afghanistan mapema leo, ameachiwa pamoja na mkalimani wake.

Gavana wa jimbo la Kunar alikotekwa mjerumani huyo, Shalizai Didar, amesema wameachiliwa huru bila masharti yoyote kufuatia mazungumzo baina ya watekaji nyara, viongozi wa kimbari na watu wengine mashuhuri katika eneo hilo.

Mwandishi wa kijerumani na mkalimani wake raia wa Afghanistan walikuwa wakichunguza mauji ya raia kadhaa kwenye shambulio la angani lililofanywa na majeshi ya jumuiya ya kujihami ya kambi ya magharibi, NATO.

Mjerumani huyo amesafiri kwenda mji mkuu wa Kunar, Asadabad, ambako atakukutana na gavana wa jimbo hilo. Hapo awali kundi la Taliban lilidai kuhusika na utekaji nyara huo.

Sambamba na hayo kundi la Taliban limemuua mateka mmoja raia wa Korea Kusini. Hapo kabla kundi hilo lilitishia kuwaua baadhi ya mateka 23 wa Korea Kusini kufikia leo saa nane ikiwa serikali ya Afghanistan haitawaachia huru wafungwa wa Taliban.