1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden aomba msaada wa NATO

P.Martin - (AFPE)10 Machi 2009

Makamu wa Rais wa Marekani, Joe Biden, amewasihi washirika wenzake katika NATO kuisaidia Marekani kupambana na uasi wa Wataliban unaozidi kushika kasi nchini Afghanistan.

https://p.dw.com/p/H9FP
U.S. Vice President Joe Biden gestures while speaking during a media conference at NATO headquarters in Brussels, Tuesday March 10, 2009. Biden is on a one-day visit to Brussels and will attend a NATO meeting and meet with EU officials. (AP Photo/Virginia Mayo)
Makamu wa Rais wa Marekani Joe Biden katika makao makuu ya NATO mjini Brussels,Ubeligiji.Picha: AP

Joe Biden,akipigia debe mkakati mpya wa serikali ya Marekani kukabiliana na hali mbaya ya usalama nchini Afghanistan, aliomba msaada wa washirika wa Nato.Amesema:

"Hali inayozidi kuwa mbaya katika kanda hiyo ni kitisho kwa kila nchi iliyowakilishwa hapa mkutanoni na sio kwa Marekani tu."

Makamu huyo wa rais wa Marekani amesema, mashambulio ya Septemba 11 yalipangwa na al-Qaeda kutoka eneo hilo. Hata mashambulio ya bomu yaliyofanywa mjini Madrid mwaka 2004 na London mwaka 2005 yalipangwa huko huko milimani kwenye mpaka wa Afghanistan na Pakistan.

Amesema,yeye amefika Brussels kusikiliza maoni ya wenzake na wasiwasi wao. Hakuja kuwashinikiza washirika wenzake kutoa ahadi za kupeleka vikosi ziada Afghanistan. Fikra alizopewa na wenzake zitajumuishwa katika mpango wa sera mpya za Marekani kuhusu Afghanistan na Pakistan. Mpango huo unatazamiwa kuwakilishwa kwa Rais wa Marekani Barack Obama kabla ya mwisho wa mwezi huu wa Machi.

Mazungumzo ya Biden pamoja na Katibu Mkuu wa NATO, Jemadari Jaap de Hoop Scheffer na mabalozi wa NATO,yamefanywa siku tano baada ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Hillary Clinton kutembelea makao makuu ya NATO mjini Brussels.Clinton alithibitisha kuwa serikali ya Obama inataka kushirikiana upya na washirika wake wa Ulaya.Hali ya usalama ikizidi kuwa mbaya nchini Afghanistan,Obama ametoa amri ya kupeleka wanajeshi 17,000 ziada wa Marekani nchini Afghanistan. Badala ya Iraq, sasa Afghanistan na Pakistan ndio zitakazopewa kipaumbele katika operesheni za kupambana na wanamgambo wenye itikadi kali za Kiislamu.

Ujerumani,Uingereza na Ufaransa zimeshasema kuwa hazitopeleka wanajeshi ziada kupigana Afghanistan. Lakini nchi za Ulaya zikifurahia mkondo mpya unaofuatwa na rais mpya wa Marekani zimesema,zipo tayari kutoa msaada wa aina nyingine kama vile kutoa mafunzo kwa vikosi vya polisi,kusaidia miradi ya kiraia na ujenzi mpya na kulinda usalama wakati wa uchaguzi wa mwezi Agosti.Ujerumani imejitolea kupeleka wanajeshi 600 ziada kuimarisha usalama,wakati wa uchaguzi huo.Takriban wanajeshi 70,000 wa kigeni wanaoongozwa na NATO na Marekani,wanapambana na uasi wa Wataliban nchini Afghanistan tangu serikali ya Taliban kutimuliwa madarakani mwisho wa mwaka 2001.