1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

GAZA:Kiongozi wa Army of Islam akamatwa na Hamas

2 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBmV

Wanamgambo wa kundi la Hamas wamemkamata kiongozi mmoja wa ngazi za juu wa kundi la Army of Islam linalohusiana na la Al Qaeda.Kundi hilo la Army of Islam ndilo linalomshika mateka mwandishi wa BBC Alan Johnstone.

Kulinga na afisa wa Hamas Sami Abu Zuhri aliyezungumza na shirika la habari la Reuters Ahmed al Mathloum aliyekuwa kaimu msemaji wa kundi la Army of Islam alikamatwa baada ya mapigano makali.

Kundi la Army of Islam linalohusishwa na koo zilizo na nguvu katika Ukanda wa Gaza limetoa kanda za video za mwandishi wa BBC Alan Johnston kupitia mtandao unaotumiwa na kundi la kigaidi la Al Qaeda. Bado haijabainika namna kundi hilo linashirikiana na kundi la Al Qaeda.Kundi la Army of Islam linataka wafungwa kuachiwa nchini Uingereza na mataifa mengine huku likitisha kumuua mwandishi huyo wa BBC aliyepotea tangu mwezi Machi endapo majeshi ya usalama yatatumia nguvu ili kuhakikisha anaachiwa huru.

Kundi la Hamas liliteka eneo la Ukanda wa Gaza majuma matatu yaliyopita na kuwafurusha majeshi ya Rais Mahmoud Abbas anayeungwa mkono na mataifa ya magharibi.Ismail Haniyeh kiongozi wa kundi la Hamas bado anajichukulia kama Waziri Mkuu japo Rais Mahmoud Abbas aliye na makao yake katika Ukingo wa Magharibi aliunda serikali ya dharura.