1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

GULU:Jeshi la Uganda laanza opresheni nyingine ya kuwasaka waasi wa LRA

4 Oktoba 2006
https://p.dw.com/p/CD6I

Jeshi la Uganda limearifu hii leo kwamba limeanzisha tena operesheni ya kuwasaka waasi wa Lords Resistance Army LRA katika eneo la kaskazini mwa nchi hiyo.

Hatua hiyo ya jeshi la Uganda inachukuliwa licha ya mazungumzo ya amani yanayolengwa kumaliza mapigano ya muda mrefu.

Msemaji wa jeshi la Uganda Meja Felix Kulaije amesisitiza kwamba operesheni hiyo haitozuia majadiliano kati ya pande mbili zinazoshiriki mazungumzo ya amani kusini mwa Sudan.

Meja Kulaije amesema hatua hii inachukuliwa kutokana na waasi hao kushindwa kukusanyika kwenye vituo viwili vilivyotengwa maalum kwa ajili yao kwa mujibu wa mapatano ya amani ambayo yalimalizika mnamo Septemba 19.

Mazungumzo ya kutafuta amani kati ya wapatanishi wa serikali ya Uganda na wajumbe wa LRA yamekuwa yakikabiliwa na utata kila mara.