Hatima ya mhandisi wa Kijerumani haijulikani
28 Julai 2007Wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani,mjini Berlin imesema,kikundi maalum cha dharura kinaendelea na juhudi zinazohusika na kuachiliwa huru mhandisi huyo.Msemaji wa wizara hiyo lakini,alikataa kutoa maelezo zaidi.
Mjerumani mwengine alietekwa nyara Afghanistan pamoja na mhandisi huyo,alifariki alipokuwa amezuiliwa mateka.Maiti yake imeletwa Ujerumani mapema juma hili.Madaktari wanaochunguza maiti hiyo wamesema,itachukua muda wa siku kadhaa kugundua kile kilichosababisha kifo cha mateka huyo.
Wakati huo huo,wanamgambo wa Taliban nchini Afghanistan, wamerefusha muda waliotoa kwa serikali,ili kumruhusu mjumbe wa Korea ya Kusini kushiriki katika majadiliano ya kuwaachilia huru mateka 22 wa Korea ya Kusini.
Mjumbe Baek Jong Chun amewasili Kabul,kujadiliana na maafisa wa Afghanistan na wajumbe wa Taliban waliotishia kuwaua mateka wa Korea ya Kusini.
Wataliban wanaitaka serikali ya Afghanistan iwaachilie huru wapiganaji wanane wa Taliban waliofungwa jela.