1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jaji Mkuu wa Pakistan amerejea kazini

P.Martin21 Julai 2007

Jaji mkuu wa Pakistan Iftikhar Mohammed Chaudhry alieachishwa kazi na Rais Pervez Musharraf, amerejea kazini hii leo akishangiriwa na mamia ya wanasheria nyumbani kwake,mjini Islamabad.

https://p.dw.com/p/CB2d
Jaji Mkuu Chaudhry akizungukwa na wafuasi wake
Jaji Mkuu Chaudhry akizungukwa na wafuasi wakePicha: AP

Mahakama Kuu ya Pakistan,imeamua kuwa hatua iliyochukuliwa na Rais Musharraf tarehe 9 mwezi wa Machi,kumfukuza kazi jaji mkuu Chaudhry,si halali.Umamuzi wa Mahakama Kuu unatazamwa kama ni pigo kwa Musharraf na mamlaka yake.

Lakini Naibu-Waziri wa habari wa Pakistan,Tariq Azim Khan ana maoni mengine.Alipohojiwa na CNN,Khan alisema,huenda ikawa nafasi ya Rais Musharraf imeimarishwa.Akaeleza kuwa kwa mara ya kwanza katika historia ya Pakistan,serikali haikuwashinikiza majaji na waliachiwa uhuru wa kuitafsiri katiba kama ipasavyo kutafsiriwa.