1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

KINSHASA : Mtafiti mkuu wa nuklea mbaroni

9 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCL4

Waziri katika serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo hapo jana amemshutumu afisa wa ngazi ya juu wa utafiti wa nuklea nchini humo aliekamatwa mapema wiki hii kwa kuwemo kwenye kundi la mtandao wa kimataifa lilioundwa kuchimba na kusafirishwa madini ya uranium kinyume na sheria kutoka nchini humo.

Profesa Fortunat Lumu ambaye ni Kamishna Mkuu wa Nishati ya Atomu nchini Congo alikamatwa wiki hii na afisa mmoja mwengine baada ya magazeti ya Kinshasa kurepoti kutoweka kwa uranium kutoka taasisi ya atomu mjini humo.

Waziri wa Utafiti wa Sayansi Sylvanus Mushi ambaye amechaguliwa hivi karibuni katika serikali mpya ya Congo amesema Lumu na mwenzake wamefanya mikataba isio halali na kampuni za kigeni bila ya ruhusa ya serikali.

Amelielezea kundi hilo lenye watu kutoka duniani kote kuanzia Ulaya,Afrika Kusini na Ushelisheli kuwa ni mtandao wa uhalifu.