1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiongozi wa upinzani wa Chad akimbilia Ufaransa

6 Machi 2008
https://p.dw.com/p/DJt5

PARIS:

Kiongozi wa upinzani wa Chad,Ngarlejy Yorongar aliekimbilia Ufaransa amesema, anahofu kuwa mwenzake anaeipinga serikali ya Rais Idriss Deby huenda ikawa ameuawa alipokuwa kizuizini.Yorongar alitoweka tangu mwezi mmoja uliopita baada ya mashambulizi ya waasi kushindwa katika mji mkuu Ndjamena.Hii leo amewasili Paris kutoka Cameroon baada ya serikali ya Ufaransa kusema ipo tayari kumpa hifadhi ya kisiasa.

Alipozungumza na waandishi wa habari kwenye uwanja wa ndege alisema,alizuiliwa na mlinzi wa Rais Idriss Deby mjini Ndjamena tarehe 3 Februari katika jela ya siri kabla ya kufanikiwa kukimbilia nchi jirani ya Cameroon.Serikali ya Chad imetangaza hali ya hatari hadi Machi 15.Amri hiyo inaruhusu majumba ya watu kusakwa na vikosi vya usalama na hatua kali kuchukuliwa dhidi ya vyombo vya habari.