Kumbukumbu ya mwaka mmoja wa tetemeko la ardhi China
12 Mei 2009Rais Hu Jintao amewaongoza wananchi wa nchi hiyo katika kumbukumbu hiyo iliyofanyika kwenye jimbo hilo la Sichuan.
Ukarabati wa eneo hilo unaendelea kwa kasi kubwa, lakini wahanga wa janga hilo, ambao walipoteza ndugu zao bado wana kabiliwa na wakati mgumu wa kuwakumbuka wapendwa wao.
Mwandishi wetu Ruth Kirchner ametembelea mji wa Beichuan ambao ulibomolewa kabisa na tetemeko hilo, na kututumia taarifa ifuatayo msimulizi studioni ni Aboubakary Liongo
Ni kumbukumbu tu tena ndogo ya mji wa Beichuan uliyoko mlimani.Harufu ya udi na ubani imetapakaa, huku upepo wa majira ya joto ukipepea mishumaa iliyowashwa.Kwa mbali Dao Zhang Cui amekaa kwenye mteremeko mlimani, kuelekea kwenye bonde ulipokuwa mji, ameonyoosha mikono yake huku akimuita mtoto wake.
´´Kipenzi changu siku chache zijazo utatimiza miaka minane.Nakukumbuka sana´´.
Sauti ya kilio chake inapaa na kusharabu, lakini hakuna jibu.Katika mabaki ya nyumba zilizobomolewa na tetemeko hilo ndiko yaliko mabaki ya mwili wa binti yake Wang Yu Quing.
Katika siku ya kumbukumbu ya kwanza toka janga hilo Dao Zhang Cui ambaye sasa anakaa mbali na hapa anasema anakwenda kwenye eneo hilo ambalo ni kaburi la binti yake, na anatamani kwenda kila siku
´´Siwezi kabisa kusahau, alikuwa msichana mzuri, nitamnunulia zawadi kwa ajili ya siku yake ya kuzaliwa siku chache zijazo.Nampenda sana mwanangu.Nyumba ya mama ambako ndiko nakoishi hivi sasa ni milimani mbali na hapa kwa kutumia pikipiki inakuchukua saa nne.Ningependa kuja kila siku kumtembelea binti yangu´´
Hii ni mara ya tatu kwa China kufanya kumbukumbu ya janga hilo la tetemeko la ardhi ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.
Mara kwanza katika siku ya mwaka mpya wa kichina, na mara ya pili ilikuwa mwezi uliyopita katika siku ya kumbukumbu ya maafa.
Hawa ni askari wa jeshi la kimapinduzi la china wanafanya mazoezi kwa ajili ya kumbukumbu hii.
Kiasi cha kilomita 15 kutoka kwenye eneo hilo kuna bango kubwa lililoandikwa, Beichuan mpya ndoto mpya.
Hata hivyo bado hakuna nyumba hata moja iliyojengwa , na inaarifiwa kuwa itachukua miaka mitatu ijayo majengo hayo kuweza kukamilika.
Lakini katika mji wa Dujiangyan kasi ya ujenzi wa makazi mapya inaendelea, na muda si mrefu familia zaidi ya elfu 3 zitahamia hapa, kama alivyonithibitishia fundi huyu wa shirika la ujenzi la serikali aitwaye Xue Tiang Tang.
´´Ujenzi ulianza Septemba mwaka jana, maeneo muhimu ikiwa ni pamoja na kupaua yameshakamilika.Mwezi decemba watu wa mwanzo wataanza kuingia Mwezi mei mwakani nyumba zote zitakuwa zimekamilika´´.
Kumbukumbu hii inafanyika katika mji huu wa Beichuan,ambapo Rais Hu Jintao alianza kutoa hutoba yake mara baada ya kimya cha kuwakumbuka wahanga saa 3.28 kwa saa za afrika mashariki muda ambao ndiyo tetemeko hilo liliukumbuka mji huu.
Watu zaidi ya milioni tano mpaka sasa hawana makaazi kutokana na madhara ya janga hilo.
Mwandishi:Ruth Kirchner/A.Liongo
Mhariri:Othman Miradji