1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Machafuko Iran yatautimua utawala wa Mamullah ?

29 Desemba 2009

je, hatua kali za usalama viwanja vya ndege zastahiki ?

https://p.dw.com/p/LG8B
Iranian yafukamotoPicha: AP

Maoni ya wahariri wa magazeti ya leo ya Ujerumani, yamechambua mada mbali mbali tangu za ndani nchini kama vile kodi za mapato na mada za nje ya nchi kama vile hatua kali za usalama zinazochukuliwa sasa baada ya njama ya kutaka kuiripua ndege ya shirika la Marekani ya mnigeria Abdulmutalib.Mada iliochambuliwa mno hatahivyo, ni machafuko ya hivi sasa nchini Iran dhidi ya utawala wa Mamullah.

Gazeti la Märkische Oderzeitung Laandika:

"Picha tunazojionea kutoka Teheran na miji mingine ya Iran, kutoka vyombo vya habari ulimwenguni , zaonesha malalamiko hasa yanafanywa na vijana .Baadhi yao ni wanafunzi na raia wa tabaka la kati na kati ambao hawana matumaini ya maisha bora nchini mwao ambako hali ya uchumi imezidi kuwa mbaya.Hawa ni vijana ambao, wangeiongoza nchi yao kuwa dola la kisasa lililoendelea kiuchumi.

Ni swali la kutatanisha kujua lini na iwapo viongozi wa usoni wa nchi hii waliogawika watajiunga na wimbi hili la maandamano na kuligeuza mapinduzi ya kweli."

Ama gazeti la RHEIN-ZEITUNG linaandika kwamba, wananchi nchini Iran hivi sasa sio tu hawachelei tena kumiminika barabarani na kutoa jasho lao kuupinga utawala wa kikatili , bali wanachochea moto wa malalamiko zaidi.Hii yaonesha:

"Utawala wa Iran , hauwatishi tena na hauwezi tena kuegemea turufu ya kuendelea kuutisha umma kwa mkomoto .Na kila machafuko yakizidi,yanakidhofisha na kukitikisa kiti cha rais Ahmadinejad."

Gazeti la Westfälische Nachrichten, linaandika kuwa, utawala wa Jamhuri ya kiislamu ya Iran ambao mamullah waliounda 1979,unaonesha unatikisika mno.Hatahivyo, badiliko la haraka la utawala huo halionekani.Gazeti laongeza:

"Laiti mkomoto ungekoma,mafanikio mengi yangepatikana. Kwa sharti kuwa,viongozi wa kidini humo nchini wanatanabahi kuwa , wanabidi kujitoa mhanga kwa kumtimua Ahmadinejad madarakani."

Likitugeuzia mada ,gazeti la NEUE Westfälische, linazungumzia hatua za usalama zilizochukuliwa hivi punde katika viwanja vya ndege mbali mbali baada ya mkasa wa kutaka kuripuliwa ndege ya kimarekani:Linaandika:

"Sio tu wamarekani bali hata wajerumani , wamejifunza darasa lao kutoka njama za kigaidi za siku za nyuma. Ujerumani,mwanzoni mwa 2005, ilipitishwa sheria ya ulinzi wa angani.Sheria hiyo ilitoa mamlaka makubwa kwa polisi nchini na idara za usalama wa anga juu ya kuwakagua abiria na mizigo yao.Hata uchunguzi wa watumishi ulifanywa kujua iwapo wanategemeka kufanya kazi zao barabara.

Likiendeleza mada hii, gazeti la Mittlebayrische Zeitung laandika kwamba, muda mfupi kabla mwaka kumalizika, mikasa 2 ya zamani imeturejea:Hofu juu ya ugaidi na na rafiki yake -hatua kali za usalama.Kwavile, mara hii imebahatika kuizima njama ambayo ingehilikisha maisha ya mamia kadhaa ya wanadamu wakati wa siku kuu za X-masi,vilio vinasikika tena kwa sauti kubwa kuwa:

"Tunahitaji usalama zaidi na bora zaidi kuwamurika watu miili yao kwa mitambo ya scanner.Wanaitisha hayo kana kwamba , zana za kiufundi pekee zingesaidia kutatua tatizo hilo. Kinachosikitisha katika mjadala huu mara nyingi, ni kutibu dalili za maradhi badala ya kutibu maradhi yenyewe au chanzo chake."

Mwandishi: Ramadhan Ali/ DPA

Uhariri: Yusuf Saumu