1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mawaziri wa kigeni wa Umoja wa Ulaya wakutana mjini Brussels

18 Februari 2008
https://p.dw.com/p/D9KB

Mawaziri wa mashauri ya kigeni wa Umoja wa Ulaya wanakutana mjini Brussels Ubelgiji kutathmini athari za hatua ya Kosovo kujitangazia uhuru kutoka kwa Serbia.

Umoja wa Ulaya umegawanyika kuhusu swala hilo huku ukijaribu kutafuta msimamo wa pamoja kuhusu nchi mpya ya Kosovo.

Uhispania inapinga kuitambua Kosovo ikihofia hatua hiyo huenda ikawapa nguvu waasi wa chama cha Basque wachukue hatua kama hiyo.

Cyprus, Bulgaria, Ugiriki, Romania na Slovakia bado zinasita kuiunga mkono Kosovo kwa sababu zinakabiliwa na matatizo ya waasi na mipaka.

Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel, amesema serikali yake haitachukua uamuzi wa haraka kuutambua uhuru wa Kosovo lakini itausubiri Umoja wa Ulaya utoe msimamo wake.

Ujerumani ilitarajiwa kuitambua rasmi Kosovo hii leo pamoja na Uingereza, Ufaransa, Italy na Marekani. Kansela Merkel amesema hofu kwamba kuitambua Kosovo huenda isababishe uchochezi haina msingi.

Kwa upande wake rais George W Bush wa Marekani amesema raia wa Kosovo sasa wako huru. Katika mahojiano yake na shirika la habari la NBC mjini Arusha nchini Tanzania rais Bush amesema Marekani itautambua uhuru wa Kosovo kwa mujibu wa mpango wa mjumbe wa Umoja wa Mataifa, Mahti Ahtisaari.