1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel aitisha mkutano kujadili mgogoro wa wakimbizi

Admin.WagnerD15 Septemba 2015

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ameitisha mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya wiki ijayo kuhusu mgogoro wa wakimbizi, akisema suluhu ya pamoja inahitajika ili kukabiliana na mgogoro huo uliyougawa Umoja wa Ulaya.

https://p.dw.com/p/1GWvo
Kansela Merkel akiwa kwenye mkutano wa waandishi na mwezake wa Austria Werner Faymann.
Kansela Merkel akiwa kwenye mkutano wa waandishi na mwezake wa Austria Werner Faymann.Picha: Reuters/Hannibal Hanschke

Merkel aliyasema hayo katika mkutano wa pamoja na kansela wa Austria Werner Faymann mjini Berlin siku ya Jumanne, huku Hungary ikitangaza hali ya hatari na kufunga mpaka wake na Serbia kuzuwia mmiminiko wa wakimbizi zaidi.

Amesema Ulaya iko katika hali ngumu sana, na kuutaja mgogoro wa wakimbizi kuwa ndiyo changamoto kubwa zaidi iliyoukumba umoja wa ulaya katika kipindi cha miongo kadhaa, huku akisisitiza kuwa changamoto hiyo itatatuliwa tu kwa matazamo sawa.

"Hili ni tatizo na Ulaya nzima na linaweza tu kutatuliwa kwa ushirikiano wa mataifa yote ya Umoja wa Ulaya. Ni jukumu la umoja wote wa Ulaya na ndiyo maana tumekubaliana kuwa na mkutano maalumu wa kilele wa Umoja wa Ulaya wiki ijayo," alisema Merkel.

Wakimbizi wakisota nje ya mpaka wa Hungary na Serbia, baada ya Hungary kukamilisha uzio wa nyenyenge kuwazuwia kukanyaga ardhi yake.
Wakimbizi wakisota nje ya mpaka wa Hungary na Serbia, baada ya Hungary kukamilisha uzio wa nyenyenge kuwazuwia kukanyaga ardhi yake.Picha: Reuters/B. Szabo

Ujerumani na Austria zilirejesha ukaguzi wa mipakani wiki hii kupunguza mtiririko wa wakimbizi wanaowasili kutoka Hungary, ambayo leo nayo imetangaza hatua za dharura kuwazuwia wahamiaji kuvuka mpaka wake na Serbia, ambako imekamilisha ujenzi wa uzio.

Ukaguzi kuendelea

Merkel amesema ukaguzi wa mipakani, ambao kimsingi unasitisha mkataba wa Schengeni kuhusu uhuru wa kusafiri katika mataifa 26 ya Ulaya, vitaendelea kuwepo hadi usalama urejeshwe. Serikali ya Ujerumani ilitangaza kurejesha kwa udhibiti wa mipakani siku ya Jumapili, baada ya maafisa kulalamika kuwa hawawezi tena kumudu mmiminiko wa wakimbizi, ambao ulivunja rekodi mwishoni mwa wiki.

Naibu Kansela Sigmar Gabriel, amesema leo kuwa Ulaya imejidhalilisha baada ya mawaziri wa mambo ya ndani kushindwa kufikia muafaka kuhusu mpango wa mgawanyo wa wakimbizi wapatao 120,000, na kusema mataifa ya Umoja wa Ulaya yanapaswa kufahamu kuwa Ulaya iko hatarini, na kwamba kinachoshuhudiwa hivi sasa kinalitishia bara hilo kuliko hata mgogoro wa madeni ya Ugiriki.

Gabriel pia amesema Umoja wa Ulaya unapaswa kuzingatia shinikizo la kifedha kwa mataifa yanayokataa kuwapokea wakimbizi.

"Ni wazi kuwa tusipofikia makubaliano, mipango w amuda wa kati ya Ulaya haitokuwa chochote zaidi ya moshi na vioo. Ujerumani haitakuwa tayari kuwa mlipaji mkuu wa Ulaya," alisema naibu huyo wa Merkel na kuongeza kuwa "kila mtu anashiriki wakipata pesa, lakini hakuna anaeshiriki linapokuja suala la kuwajibika. Huo ndiyo utakuwa mwisho wa msingi wa ufadhili ikiwa hali hii itaendelea."

Czech, Slovakia zaibeza Ujerumani

Matumaini ya kufikiwa muafaka wa kugawana wakimbizi 120,000 kutoka mataifa yaliyozidiwa ya Ugiriki, Italia na Hungary, miongoni mwa mataifa yote wanachama wa Umoja wa Ulaya, yalififia siku ya Jumatano kutokana na upinzani mkali kutoka kwa Hungary yenyewe, Jamhuri ya Czech, Slovakia na Romania.

Naibu Kansela wa Ujerumani Sigmar Gabriel.
Naibu Kansela wa Ujerumani Sigmar Gabriel.Picha: picture-alliance/dpa/W. Kumm

Lakini afisa wa serikali ya Jamhuri ya Czech ameikosoa Ujerumani kwa kile alichosema ni kutoa vitisho visivyo na mashiko, huku Slovakia ikisema ikiwa vitisho hivyo vitatekelezwa basi huo ndiyo utakuwa miwsho wa Umoja wa Ulaya.

Serikali ya mrengo mkali wa kulia nchini Hungary, imefunga njia kuu ya kuingilia wakimbizi kutoka nchini jirani ya Serbia leo, kukataa maobi 16 ya hifadhi, huku watu 171 wakiripotiwa kukamatwa wakati wanajaribu kuvuka mpaka kinyume na sheria.

Wakati huo huo, Uswisi imesema itakubali viwango vya mgawanyo wa wakimbizi vilivyopendekezwa na Umoja wa Ulaya, amesema rais wake Simonetta Sommaruga, huku rais wa Slovenia Borut Pahor naye akielezea kuunga mkono mpango huo, huku akisema mgogoro wa wakimbizi unaweza kuwa changamoto kubwa zaidi kwa Umoja wa Ulaya kuliko mgogor wa kifedha uliyoanza mwaka 2008.

Mwandishi: Iddi Ssessanga/afpe,dpae,ape,rtre.

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman