1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Musharraf kuacha kuwa mkuu wa jeshi.

21 Novemba 2007
https://p.dw.com/p/CQ1v

Islamabad.

Rais wa Pakistan Pervez Musharraf anatarajiwa kuacha madaraka ya mkuu wa jeshi la nchi hiyo na kuwa rais wa Kiraia mwishoni mwa juma hili wakati kiongozi huyo wa kijeshi akipata uungwaji mkono zaidi kutoka Marekani. Mwanasheria mkuu wa serikali Malik Mohammed Qayyum ameliambia shirika la habari la AFP leo, kuwa iwapo mahakama kuu itatupilia mbali kikwazo cha mwisho hapo kesho katika njia ya Musharraf kuchaguliwa tena kama inavyotarajiwa , ataacha sare zake za kijeshi katika muda wa siku chache.

Kiongozi huyo wa Pakistan amekuwa katika mbinyo mkubwa wa kimataifa ukiongozwa na Marekani kuondoa sheria ya hali ya hatari aliyoiweka hapo Novemba 3, aache madaraka ya mkuu wa jeshi, aitishe uchaguzi huru na kuwaachia huru wafungwa wa kisiasa. Mwanasheria mkuu amesema uchaguzi nchini humo utakuwa huru na wa haki.

Mwanasheria mkuu amesisitiza kuwa iwapo mahakama kuu itaondoa amri ya kumzuwia dhidi ya kuchaguliwa kwake tena kuwa rais, rais Musharraf anaweza kuapishwa kama rais wa kiraia ifikapo Jumamosi ama Jumapili.

Wakati huo huo majeshi ya Pakistan yameshambulia eneo la wapiganaji wa Taliban katika eneo la kaskazini magharibi, na kuua waasi 40, jeshi limesema leo.