1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Barrak Obama aanza Kazi

Eric Kalume Ponda21 Januari 2009

Marekani sasa inakiongozi mpya, Rais Barack Hussein Obama.

https://p.dw.com/p/GdTR
Rais Barrak Obama wakati wa sherehe za kutawazwa.Picha: AP



Barack Obama alikula Kiapo kuwa rais wa 44 wa Marekani mbele ya mwanasheria mkuu wa mahakama kuu ya Marekani John Roberts katika sherehe iliyohudhuriwa na zaidi ya watu millioni mbili waliomiminika katika viwanja vilivyo karibu na bunge mjini Washington DC na mamilioni ya wengine duniani kote wakikusanyika kuangalia tukio hilo lililokuwa na msisimko mkubwa wa aina yake.


Ni siku iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu kote ulimwenguni kumuona kiongozi huyo mwenye haiba kubwa akianza kazi aliyoahidi wakati wa kampeini zake katika kubadilisha sura ya Marekani usoni mwa Ulimwengu.


Wazee kwa vijana,wake kwa waume,weusi na weupe hakuna aliyebakia nyuma.Kulikuwa na usalama wa hali ya juu kote.Katika Hotuba yake ambayo ilikuwa inasubiriwa kwa hamu na wengi Rais Obama hakusita kuzungumzia hali ngumu ya Uchumi nchini Marekani hadi changamoto za siasa ya nje inayolikabili taifa hilo kutokana na vita nchini Iraq na Afghanistan.

Rais Barrak Obama alisema ´Changamoto zinazotukabili ni dhahiri, ngumu na nyingi, haziwezi kutatuliwa kwa urahisi, na kwa muda mfupi. Lakini Wamarekani kuweni na ya kini yatatanzuliwa`.


Hakuna muda wa kupoteza, tayari Rais Barrak Obama ameanza kazi yake masaa 24 baada ya kuapishwa kwa kutangaza kusimamishwa kwa muda wa siku 120 kesi zote za watuhumiwa katika gereza la Guantanamo. Kwa kuzingatia umuhimu aliolipa suala la Guantanamo ni dhahiri sifa ya gereza hilo imekuwa ikimkosesha usingizi Rais Barrak Obama.


Zaidi ya watuhumiwa 800 wake kwa waume vijana kwa wazee wamepitia gereza hilo ,lililofunguliwa Januari 11 mwaka wa 2002. Hadi sasa kuna zaidi ya watuhumiwa 254 wanaozuiliwa katika gezera hilo wengi wao wakiwa hawajafikishwa mahakani.

Barrak Obama amesema kuwa atalifunga gereza hilo la Guantanamo.


Aidha aliwakumbusha wamarekani kwamba umewadia wakati wao wa kusimama upya, kujifuta vumbi na kuanza tena kazi ya kuijenga Marekani.Rais Obama ambaye ana asili ya Kenya hakusita kuzikosoa sera za mtangulizi wake Goerge W Bush kuelekea vita dhidi ya Ugaidi na uchumi na kuuambia Ulimwengu kwamba sasa Marekani iko tayari kuongoza tena.


Kadhalika ameahidi kuimarisha uhusiano na ulimwengu wa kiisalmu ambao umekuwa ukitia mashaka tangu kutokea mashambulio ya septemba 11 na pia kuwaonya viongozi wasiopenda amani wanaosababisha mizozo kwenye nchi zao na kuyatwika lawama mataifa ya magharibi.

Viongozi mbali mbali wa dunia bado wanaendelea kutoa pondezi kufuatia kuapishwa kwake kuwa rais wa Marekani. Katika risala zake za pongezi kwa rais Obama Kansela Angela Merkel wa Ujerumani amesema nchi yake iko tayari kushirikiana kwa karibu na Marekani kwa hali yoyote.



Ponda/Reuters