1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Mbeki azuru Zimbabwe kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa huko

Kalyango Siraj9 Mei 2008

Lakini haijulikani lini duru ya pili ya uchaguzi itafanywa

https://p.dw.com/p/DxGk
Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe anashinikizwa na jamii ya kimataifa kuweka mazingira huru katika duru ya pili ya uchaguzi wa urais.Pia anatakiwa kuwahimiza wafuasi wake kuacha kuwanyanyasa wafuasi wa upinzani.Picha: AP

Zimbabwe inashinikizwa kukubali wachunguzi wa kigeni katika duru ya pili ya uchaguzi wa urais nchini humo huku kukiwa na madai ya kuwa magenge ya wanamgambo wanaoiunga mkono serikali yanatoa vitisho.

Nae mpatanishi mkuu wa mgogoro wa nchi hiyo rais Thabo Mbeki wa Afrika Kusini amekwenda Zimbabwe kutekeleza kazi zake za upatanishi.

Safari ya Ijumaa ya Bw Mbeki mjini Harare,ndio ya kwanza tangu kutolewa kwa matokeo ya uchaguzi mkuu ambayo yamezusha mvutano miongoni mwa washika dau.

Mbeki,ambae amekoseolewa sana kutokana na kumdekeza cheo somo wake wa Zimbabwe,Robert Mugabe,alitarajiwa kukutana nae,lakini haikubainika mapema ikiwa pia atakutakana na upande wa upinzani.

Chama cha upinzani cha Movement for Democratic Change MDC ambacho kilishinda udhibiti wa bunge katika uchaguzi wa machi 29,na kiongozi wake Morgen Tsvangirai kumbwaga Mugabe katika duru ya kwanza ya uchaguzi,kilitaka Bw Mbeki avuliwe wadhifa wake kama mpatanishi wa mgogoro huo.

Juhudi hizi mpya za upatanishi zinakuja huku kukiwa na madai ya kuendelea kwa ghasia nchini humo ambazo zinalaumiwa kufanywa na magenge ya kimgambo yanayounga mkono serikali ya Mugabe.

Upinzani unasema kuwa kufikia sasa wafuasi wao 30 wameuawa katika sehemu mbalimbali za nchi hiyo.Huku mkuu wa chama cha wafanyakazi anasema kuwa wafanya kazi wa mashambani pamoja na familia zao takriban,elf 40 wameachwa bila ya makazi,ingawa wahusika wamepuuza kiwango cha ghasia kinachoendelea.

Mambo yanazidi kuwa magumu kutokana na hali ya sasa ambapo zikiwa zimepita siku sita tangu matokeo ya uchaguzi yatangazwe na kuhitajika duru ya pili, lakini hadi leo hiajaeleweka lini duru hiyo ifanwe ama ikiwa chama cha MDC kitashiriki.Kiongozi wake ambae kwa sasa yuko nje ya nchi ametoa tu masharti kadhaa kuhusu suala hilo.

Nayo jamii ya kimataifa imezidisha shinikizo lake kwa utawala wa Zimbabwe kukubali wachunguzi wa kigeni.Mwanabalozi mmoja wa Uingereza John Sawers alisema ikiwa duru ya pili itafanyika inafaa kuwepo na wachunguzi wa kigeni.

Naye katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki -moon katika taarifa yake amesema kuwa ni lazima mazingira yawe huru katika duru ya pili.

Msemaji wa baraza la usalama wa taifa la marekani, Gordon Johndroe amesema kuwa Mugabe na wafuasi wake wanafaa kuacha visa vya fujo dhidi ya wale wanaounga mkono upande wa upinzani.

Waziri mkuu wa Uingereza Gordon Brown nae amekariri mwito wa jamii ya kimataifa kuhusishwa kikamilifu katika duru ya pili.