1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rasimu ya Mpango wa Kuyalinda Mazingira Yapatikana Paris

5 Desemba 2015

Hatua kubwa imepigwa katika mazungumzo ya Umoja wa Mataifa kuhusu mazingira unaoendelea mjini Paris, kutafuta makubaliano ya kudumu yatakayopunguza kasi ya mabadiliko ya tabianchi na kuyanusuru mazingira ya dunia.

https://p.dw.com/p/1HHxx
Kukithiri kwa kiwango cha gesi ya Kaboni kunalaumiwa kwa ongezeko kubwa la joto duniani
Kukithiri kwa kiwango cha gesi ya Kaboni kunalaumiwa kwa ongezeko kubwa la joto dunianiPicha: picture-alliance/dpa/Ccfdcb

Wataalamu kutoka nchi 195 wamewasilisha rasimu ya mpango makhususi wa makubaliano yanayonuia kuhakikisha usalama wa mazingira ya dunia kutokana na hewa chafu inayochochea mabadiliko ya tabia nchi.

Licha ya kukabiliwa na mapendekezo yanayokinzana, rasimu ya mpango iliyowasilishwa mchana (05.12.2015) itaweka msingi muhimu zaidi kuwahi kujaribiwa kuelekea makubaliano ya dunia kuhusu udhibiti wa mabadiliko ya tabia nchi.

Jumatatu ijayo, mawaziri kutoka kote duniani watawasili katika mji mkuu wa Ufaransa, Paris, kuifanya rasimu hiyo kuwa makubaliano yenye uzito wa kisheria, utakaoweka kikomo katika utoaji wa gesi ya kaboni, ambayo hulinasa joto la jua na kusababisha ongezeko la joto katika maeneo ya nchi kavu na baharini.

Haiwezekani, hadi itakapokuwa imefanyika

Akizungumza baada ya kupatikana kwa mpango huo, mwakilishi wa Afrika Kusini Nozipho Mxakato-Diseko amenukuu maneno ya marehemu Nelson Mandela, kwamba ''Mara zote kazi itaonekana kama haiwezi kufanyika, hadi pale itakapokuwa imefanyika'', kauli ambayo imeshangiliwa mkutanoni.

Watalaamu wamefanya kazi kubwa kuafikia juu ya rasmu ya mpango mahsusi wa mazingira
Watalaamu wamefanya kazi kubwa kuafikia juu ya rasmu ya mpango mahsusi wa mazingiraPicha: Reuters/S. Mahe

Wataalamu wameonya kuwa ongezeko hilo la joto linaweza kusababisha majanga makubwa, yakiwemo kuongezeka kwa kina cha bahari, vimbunga na ukame wa muda mrefu.

Kusitisha kupanda huko kwa joto kutahitaji kusitisha matumizi ya nishati itokanayo na makaa ya mawe, bidhaa za petroli na gesi, na pia kuacha kuiangamiza misitu inayotunza gesi aina ya kaboni. Hayo ni mambo magumu na yenye gharama kubwa, ambayo makampuni ya biashara hayapendi kuyatekeleza.

Watu maarufu duniani wapatao 50, wakiwemo nyota wa filamu na mabilionea walifika mjini Paris, kusaidia kushawishi kupatikana kwa makubaliano ya kudhibiti mabadiliko ya tabia nchi.

Somo kutokana na mikutano iliyopita

Wataalamu katika mkutano huo wana matumaini ya kuepuka hali iliyojitokeza katika mkutano mwingine wa Umoja wa Mataifa kuhusu mazingira uliofanyika mjini Copenhagen mwaka 2009, ambayo yalinuia kupata makubaliano ifikapo mwaka 2012, ambayo hata hivyo yalifeli na kuvunjika.

Vimbunga na mafuriko ni miongoni mwa majanga yatokanayo na ongezeko la joto duniani
Vimbunga na mafuriko ni miongoni mwa majanga yatokanayo na ongezeko la joto dunianiPicha: picture alliance/ZUMA Press/Jashim Salam

Miaka miwili baada ya kushindwa kwa mkutano huo wa Copenhagen, mwaka 2011, wataalamu wa kimataifa walikutana mjini Durban na kukubaliana kupata mpango mwingine wa kuyanusuru mazingira ya dunia.

Kwa mujibu wa watalaamu mbali mbali, makubaliano yatakayotokana na mkutano wa Paris yatakuwa na mapungufu ya vigezo vinavyohitajika, kuweza kuzuia ongezeko la joto duniani kwa zaidi ya nyuzi 2, juu ya kiwango kilichokuwepo kabla ya mapinduzi ya viwanda.

Bado kuna tofauti kubwa kuhusu masuala muhimu, kama vile kiwango cha upunguzaji wa hewa chafu inayochafua mazingira, upande utakaojitwisha juhumu kubwa ya mchakato huo na muhimu zaidi, nani ataugharimia mchakato huo.

Mwandishi: Daniel Gakuba/afpe/ape

Mhariri: Caro Robi