1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

THE HAGUE :Taylor adai kutopata uamuzi wa haki

4 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBup

Rais wa zamani wa Liberia Charles Taylor amekataa kufika mahakamani katika ufunguzi wa kesi yake ya uhalifu wa kivita.Katika waraka wake uliosomwa mahakamani na wakili wake Karim Khan,Bwana Taylor anasusia kikao hicho kwa kuamini kuwa hatatendewa haki katika mahakama hiyo maalum.Kwa upande wake anadai kuwa ana mtetezi mmoja pekee ikilinganishwa na tisa wa upande wa mashtaka.

Mwendesha mashtaka mkuu Stephen Rapp alielezea mahakama hiyo uhalifu alioutenda Bwana Taylor wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu miaka 11 nchini Sierra Leone.

Bwana Taylor ni kiongozi wa kwanza wa taifa barani Afrika kujibu mashtaka ya uhalifu wa kivita mbele ya mahakama ya kimataifa.Kwa mujibu wa mashtaka yanayomkabili Bwana Taylor aliwafadhili na kuwapa mafunzo na silaha waasi wa Revolutionary United Front, RUF wanaodaiwa kutekeleza vitendo vyote vya kikatili ili kupata almasi.Taylor kwa upande wake anakanusha madai yote hayo.