1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa ulaya wamshinikiza rais wa jamhuri ya Cheki Vaclav Klaus

Oumilkher Hamidou14 Oktoba 2009

Rais wa jamahuri ya Cheki ang'ang'ania msimamo wake dhidi ya kutia saini mkataba wa Lisbon

https://p.dw.com/p/K69e
Waziri mkuu wa Cheki Jan Fischer na mwenyekiti wa halmashauri kuu ya umoja wa ulaya BarrosoPicha: AP

Jamhuri ya Tcheki ni ya mwisho kati ya wanachama 27 wa Umoja wa Ulaya,ambayo hadi sasa haijatia saini bado mkataba wa Lisbon.Mwenyekiti wa halmashauri kuu ya umoja wa ulaya Jose Manuel Barroso ameionya serikali ya mjini Prague jana,watapoteza wadhifa wao mmoja wa kamishna wa umoja wa ulaya,ikiwa rais Vaclav Klaus ataendelea kupinga kutia saini mkataba huo.

Baada ya mazungumzo pamoja na waziri mkuu wa jamhuri ya Tcheki,jana mjini Bruxelles,mwenyekiti wa halmashauri kuu ya umoja wa Ulaya Jose Manuel Barroso amesema anataraji hata hivyo jamhuri ya Tcheki itatekeleza wajib wake.

Sura za viongozi hao wawili zimedhihirisha jinsi kishindo kilivyo kikubwa.Lakini mhusika hasa hajakuwepo mazungumzoni;yaani rais wa jamhuri ya Tcheki Vaclav Klaus.Na huyo hasa ndie aliyekusudiwa matamshi ya mwenyekiti wa halmashauri kuu ya Umoja wa ulaya,Jose Manuel Barroso.

Tschechien EU Vaclav Klaus Pressekonferenz in Prag
Rais Vaclav Klaus wa jamahuri ya ChekiPicha: AP

"Tunajikuta katika hali ambayo mwanachama mmoja anakabiliana na wanachama wote waliosalia pamoja na kukabiliana na taasisi zote za Umoja wa ulaya.Na hili ni jukumu kubwa kupita kiasi."

Kwanza mahakama ya katiba ya jamhuri ya Tcheki itabidi ipitishe uamuzi wake kuhusiana na mashtaka yaliyotumwa.Hata hivyo Barroso anaamini mahkama hiyo ya katiba itaunga mkono mkataba wa Lisbon kama ilivyofanya hapo awali.Hapo tena itakua tena zamu ya rais Vaclav Klaus kuamua .Mzigo mkubwa zaidi anaubeba waziri mkuu Jan Fischer.Yeye binafsi anaunga mkono mkataba wa Lisbon na kwa wiki kadhaa sasa amekua akimsihi Klaus akubali kutia saini mkataba huo.Lakini ilikua kazi bure.

Akiwa ziarani Barvikha,karibu na mji mkuu wa Urusi Moscow,rais Vaclav Klaus amesema hii leo hayuko tayari kudalisha msimamo wake kuhusiana na mkataba wa Lisbonn.

Katika mazungumzo na waandishi habari pamoja na rais Dmitri Medvedev wa Urusi,rais Klaus anasema masharti aliyotoa ili kutia saini mkataba wa Lisbon ni muhimu.Rais Vaclav Klaus anahofia kwa kutia saini mkataba wa Lisbonn wacheki wenye asili ya Ujerumani waliotimuliwa nchini humo,wanaojulikana kama Sudetendeutsche,wasije wakadai warejeshewe milki zao.

Mwanasiasa wa Ujerumani anaeshughulikia masuala ya Ulaya Elmar Brok ameshasema mkataba wa Lisbonn hauhusiani hata kidogo na suala hilo.

Elmar Brok ,sawa na wanasiasa wengi wengine wanaamini rais Vaclav Klaus anaitumia tuu hoja hiyo kama kisingizio cha kutosaini mkataba wa Lisbonn.

Kimsingi mwenyekiti wa halmashauri kuu ya umoja wa ulaya,Jose Manuel Barroso hapingi madai ya rais wa jamhuri ya Tcheki.Lakini la muhimu hapo ni jinsi ya kuyatekeleza.Mwishoni mwa mwezi huu,viongozi wa taifa na serikali wanatazamiwa kukutana na huenda wakatoa taarifa kuhusu kizungumkuti hiki.

Mwandishi:Hasselbach,Christoph(DW Brüssel)/Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Abdul-Rahman