1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN yasema kesi dhidi ya viongozi wa Kenya itaendelea

Mjahida16 Novemba 2013

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limetupilia mbali ombi la Umoja wa Afrika kutaka kuahirishwa kwa mwaka mmoja kesi dhidi ya Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, na naibu wake William Ruto, katika mahakama ya ICC.

https://p.dw.com/p/1AIe8
Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa MataifaPicha: Reuters

Ombi la serikali ya Kenya la kutaka kuahirishwa kwa kesi hiyo ya uhalifu halikukubalika baada ya wanachama 7 kati ya 15 waliopiga kura kukataa ombi hilo.

Nchi nane wanachama wa baraza hilo hazikushiriki katika zoezi hilo. Angalau kura takriban tisa zilihitajika ili kupita kwa azimio hilo lililotolewa na Umoja wa Afrika.

Rwanda, Togo, Morocco, China, Urusi, Pakistan na Azerbaijan ndizo nchi zilizounga mkono azimio hilo huku Marekani, Uingereza, Ufaransa, Guatemala, Argentina, Australia, Luxembourg na Korea Kusini zikijitoa katika zoezi la kupiga kura.

Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Samantha Power
Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Samantha PowerPicha: picture alliance/AP Photo

Kulingana na Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Samantha Power masuala yalioibuliwa juu ya kuendelea kwa kesi hiyo katika mahakama ya ICC yanapaswa kutatuliwa zaidi na mahakama yenyewe kuliko baraza hilo.

"Familia ya waathirika wa ghasia za baada ya uchaguzi mwaka wa 2008 nchini Kenya tayari wameshasubiri kwa zaidi ya miaka mitano kwa mahakama kuanza kupima ushahidi unaotolewa mbele yake," alisema Samantha Power.

Balozi huyo pia amesema kwamba wanaamini haki kwa waathirika ni muhimu kwa taifa la Kenya kuwa na amani na usalama wa kudumu.

Viongozi kusimama katika Mahakama ya ICC

Rais Uhuru Kenyatta ambaye alichaguliwa kuliongoza taifa hilo la Afrika Mashariki, katika uchaguzi uliofanyika Machi 4 mwaka huu, anapaswa kusimama katika mahakama ya uhalifu wa kivita ICC kujibu mashtaka dhidi yake ya kupanga ghasia za baada ya uchaguzi.

Ghasia hizo zinadaiwa kufanyika wakati wa uchaguzi uliokuwa na utata wa mwaka 2007/2008 nchini Kenya ambapo zaidi ya watu 1200 waliuwawa na wengine zaidi ya laki tano wakiachwa bila makao.

Makamu wa Rais William Ruto na Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta
Makamu wa Rais William Ruto na Rais wa Kenya Uhuru KenyattaPicha: picture alliance/dpa

Azimio hilo lilillowasilishwa kwa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa lilitaka kesi hiyo iahirishwe kwa mwaka mmoja ili kuzuia hofu yakutokea kwa ghasia nchini Kenya na hata vitisho vya Ugaidi, hasaa wakati ambapo hivi maajuzi jengo la biashara la Westgate mjini Nairobi lilitekwa nyara na kundi la kigaidi la Al shabaab hatua iliyosababisha mauaji ya takriban watu 67.

China yaunga mkono azimio

Balozi wa china Liu Jieyi, ambaye pia ni rais wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa amesema nchi yake imepiga kura ya kukubali azimio lililoungwa mkono na Umoja wa Afrika ulio na nchi wanachana 54 .

"Mataifa ya Afrika yametoa hoja nzito sana zinazojisimamia, kwa hiyo ni muhimu kwa baraza hili kuunga mkono hoja hizo zinazohusu amani usalama na kukabiliana na ugaidi." Alisema Balozi Liu Jieyi.

Hata hivyo Kenya imeiita kura hiyo, kura ilioshindwa huku ikilishutumu baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kuchukua uongozi wa dunia nzima kiholela.

Majaji katika mahakama ya uhalifu ya ICC
Majaji katika mahakama ya uhalifu ya ICCPicha: AP

Kenya imesema katika taarifa yake kwamba, Umoja wa Afrika kwa sauti moja wamechukua hatua iliohitajika kwa kupeleka ombi hilo katika baraza hilo, ikitilia maanani usalama na udhabiti inayotaka kufanikisha katika bara la Afrika lakini baraza hilo limeshindwa kufanya hivyo na kuliaibisha bara la Afrika pamoja na viongozi wake.

Huku kesi ya Rais Uhuru Kenyatta ikitarajiwa kuanza rasmi mwezi wa Februari mwaka ujao majaji wa mahakama ya ICC wameamua kwamba rais huyo atahudhuria kikao cha kwanza na kile cha mwisho katika kesi hiyo na mashahidi ndio watakaohitajika kuwepo kwa wakati mwingi katika kesi hiyo.

Mwandishi: Amina Abubakar/dpa

Mhariri: Sekione Kitojo