1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uteuzi wa mgombea urais Marekani

6 Februari 2008
https://p.dw.com/p/D39s

WASHINGTON:

Nchini Marekani kinyanaganyiro kilichoitwa Super Tuesday ambapo majimbo 24 kutoka 50 yalipiga kura kumteua yule atakaemrithi Rais George W.Bush,kimefikia kilele chake.Wajumbe wa Demokratik na Republikan watakutana mwezi Agosti na Septemba kumteua rasmi yule atakaegombea urais katika uchaguzi uliopangwa kufanywa mwanzoni mwa mwezi Novemba.

Matokeo ya mwanzo ya kinyangányiro cha siku ya Jumanne yanaonyesha kuwa wagombea urais wa Demokratik,Seneta Barack Obama na Hillary Clinton wanakwenda bega kwa bega.Upande wa chama cha Republikan yadhihirika kuwa Seneta John McCain anaungwa mkono na raia wenye misimamo ya wastani wakithamini uongozi na uzoefu wa mwanasiasa huyo.Mpinzani wake Mitt Romney amesomba kura za wahafidhina na wale wanaotaka kuona hatua kali zikichukuliwa dhidi ya wahamiaji wanaoishi Marekani kinyume cha sheria.