1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapiganaji wa Al Shabab nchini Somalia, waanzisha utawala wa sharia.

Halima Nyanza/(Reuters) 27 Januari 2009

Kundi la wapiganaji wa Al Shabab leo limeanzisha utawala wa sharia za Kiislamu katika mji wa Baidoa, siku moja baada ya kuchukua mamlaka ya mji huo, ambao ulikuwa nguzo kubwa ya Serikali ya mpito ya Somalia.

https://p.dw.com/p/GhJF
Hawa ni wanajeshi wa Ethiopia waliondoka Somalia, ambapo siku moja baadaye wapiganaji wa Al Shabaab wakauteka mji wa Baidoa, ngome ya serikali ya mpito.Picha: picture-alliance/ dpa

Wapiganaji wa Kundi la Al Shabab, ambalo Marekani imeliweka katika orodha yake ya makundi ya kigaidi, jana waliuteka mji wa Baidoa, siku moja baada Majeshi ya Ethiopia yaliyokuwa yakiisaidia serikali ya mpito ya nchi hiyo, kuondoka kabisa nchini humo, baada ya miaka takrtiban miwili toka kuingia nchini humo na kukabiliwa na upinzani mkubwa.

Mara tu baada ya kuudhibiti mji huo ukiwemo uwanja wa ndege, majengo ya bunge na makazi ya Rais wapiganaji hao waliwataka wakaazi wake kujumuika leo katika Uwanja wa Mpira ili kuwaelezea jinsi watakavyotawala, ambapo Msemaji wa Al Shabab Sheik Muktar Robow aliwaambia mamia ya watu uwanjani humo kwamba wataubadilisha mji huo, na kutawala kwa sheria za kiislamu huku wakiwataka raia kuwa watulivu.


Mji wa Baidoa ni mahala lilipo bunge la mpito la Somalia , na kwamba wapiganaji hao, waliuteka mji huo, baada ya mapigano mafupi na majeshi ya serikali.


Hatua ya kundi hilo la Al Shabaab kuuteka mji huo wa Baidoa, kumelirejesha kundi hilo mbele ya jamii, baada ya kundi hilo kuonekana kukosa kuungwa mkono miongoni mwa watu, kutokana na mbinu zake kali zinazotumia pamoja na kupoteza ardhi kwa kundi lingine la kiislamu lenye msimamo wa kati.


Kundi la Al Shabab limekua likiongeza mamlaka yake hatua kwa hatua, wakati serikali dhaifu ya mpito ikizidi kuonyesha ishara ya kuporomoka.


Kwa sasa serikali inadhibiti eneo la mji wa Mogadishu, ingawa hata huko pia inakabiliwa na mashambulio ya mara kwa mara kutoka kwa wapiganaji.


Kutekwa kwa mji huo pia kumeliwekea kikwazo kwa bunge la nchi hiyo, ambalo linakutana wiki hii katika nchi jirani ya Djibouti.


Wiki hii Wabunge walipiga kura kulipanua bunge hilo ili kuliingiza kundi la Kiislamu lenye msimamo wa kati katika jaribio la kuunda serikali ya pamoja, ambapo pia wanatarajiwa kuchagua Rais wa nchi, chini ya mpango wa amani wa Umoja wa Mataifa, ambapo jana wabunge walipiga kura kuongeza muda wa kumchagua Rais ili kuwawezesha wabunge wapya 200 kuapishwa na kuunda kamati ya uchaguzi, ambapo Spika wa bunge hilo ambaye pia ni rais wa mpito Sheikh Aden Madobe aliarifu kuwa watachagua rais katika kipindi cha siku tano, iwapo watamaliza kazi hiyo kwa siku mbili.


Umoja wa Mataifa umekuwa ukishinikiza uchaguzi ufanyike siku kesho na na unataka rais mpya awe alau ameshachaguliwa ifikapo mwishoni mwa juma, , ili aweze kuhudhuiia Kikao chaViongozi wa Umoja wa Afrika kitakachoanza Jumapili ijayo.