1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMisri

Je, uchaguzi wa rais Misri utaleta mabadiliko yoyote?

6 Oktoba 2023

Uchaguzi wa Misri hauna dalili zozote za kubadili hali ya mambo. Hata hivyo, kampeni za kumuunga mkono rais wa sasa Abdel Fattah el-Sissi zimeanza, kama ambavyo umeanza ukandamizaji dhidi ya upinzani.

https://p.dw.com/p/4XAs6
Misri Giza | Uchaguzi wa Rais | Wafuasi wa Rais Abdel Fattah al-Sisi
Misri imo katika hali ya uchaguzi ya boti zenye picha za rais Abdel-Fattah El-Sissi zinashiriki maandamno kwenye Mto Nile, mjini Cairo, Oktoba 2, 2023, kuunga mkono ugombeaji wake katika uchaguzi wa rais wa Desemba.Picha: Amr Abdallah Dalsh/REUTERS

Haikuchukua muda mrefu kwa Misri kuingia katika hali ya uchaguzi. Siku chache tu baada ya tangazo kwamba uchaguzi wa rais ungefanyika kuanzia Desemba 10 hadi 12, na sio mwaka 2024 kama ilivyopangwa awali, mabango na vipeperushi vyenye picha za Rais wa Misri Abdel Fattah el-Sissi vilianza kuchukua nafasi ya matangazo ya mauzo katika mitaa maarufu.

Wadadisi wa mambo hawana shaka kuwa rais huyo mwenye umri wa miaka 68 atasalia madarakani, ingawa wanasiasa wengine saba wametangaza nia yao ya kugombea, na tarehe ya mwisho ya wagombea wengine kuingia kwenye kinyang'anyiro hicho itakuwa Oktoba 14.

"Wagombea wengine hawana nafasi ya kushinda uchaguzi, kwa sababu hakuna fursa kwao kushindana," Timothy E. Kaldas, naibu mkurugenzi wa Taasisi ya Tahrir ya Sera ya Mashariki ya Kati yenye makao yake mjini Washington, aliiambia DW.

Kwa hakika, wagombea wawili watarajiwa wa upinzani, Ahmed Altantawy, mkuu wa zamani wa Chama cha mrengo wa kushoto cha al-Karama (Hadhi), na Gameela Ismail, mwenyekiti wa chama cha kiliberali cha al-Dostour (Katiba), waliripoti kuwa wafuasi wao walikuwa wakinyanyaswa, kuhojiwa na, katika kesi ya Altantawy, pia kuzuiliwa.

Soma pia: Rais wa Misri el-Sissi aahidi kuwalinda wananchi maskini

Taasisi ya ushauri ya Egyptian Initiative for Personal Rights (EIPR) yenye makao yake makuu mjini Cairo, ilithibitisha kuwa ukandamizaji dhidi ya wafuasi wa Altantawy "umeongezeka, na angalau wanachama 73 wa kampeni yake wakizuiliwa kwa tuhuma za kujiunga na kikundi cha uasi au kigaidi, kueneza habari za uongo, na kutumia vibaya mitandao ya kijamii."

"Walihojiwa kwa sababu tu ya kujaza fomu za kujitolea katika kampeni ya urais ya El Tantawy, wakati wengine walipenda ukurasa wa Facebook wa kampeni hiyo,"iliongeza taasisi hiyo.

Mamlaka ya Kitaifa ya Uchaguzi ya Misri, ambayo inasimamia mchakato wa uchaguzi wa nchi hiyo, ilijibu katika taarifa kwamba madai hayo "ni madai yasiyo na msingi na ya uongo."

Misri, Giza | Uchaguzi wa Rais| Wafuasi wa Rais Abdel Fattah el-Sissi
Rais wa Misri Abdel-Fattah El-Sissi anawania muhula wa tatu.Picha: Amr Nabil/AP Photo/picture alliance

Wakati huo huo, Mada Masr, tovuti ya mwisho ya habari isiyodhibitiwa na serikali ya Misri, iliripoti kwamba simu ya Altantawy ilidukuliwa mara nyingi katika miezi iliyopita.

Udhibiti wa madara wa El-Sissi nchini Misri

"Kuna sababu ndogo sana ya kuamini kwamba uchaguzi huu utaonekana tofauti na ule wa 2018," Alice Gower, Mkurugenzi wa Siasa za Kimaeneo na Usalama katika taasisi ya ushauri ya Azure Strategy yenye makao yake makuu London, aliiambia DW.

Katika uchaguzi wa 2018, el-Sissi alishinda kwa asilimia 97 dhidi ya mpinzani mmoja mshirika baada ya wagombea wanne wa upinzani kukamatwa au kuamua kujiondoa kwa sababu ya vitisho na manyanyaso.

El-Sissi amekuwa madarakani tangu mwaka 2013 baada ya kuongoza mapinduzi ya kijeshi yaliyomng'oa madarakani Mohammed Morsi wa kundi la Udugu wa Kiislamu, aliyechaguliwa kidemokrasia baada ya vuguvugu la mabadiliko katika mataifa ya Kiarabu mwaka 2011. Chaguzi mbili zimefanyika tangu hapo, mwaka 2014 na 2018, lakini waangalizi wa mambo wanakosoa kwamba zote mbili zilikosa usawa.

Soma pia: Misri: Ukandamizaji waendelea licha ya kuachiwa wanaharakati

Mnamo 2019, El-Sissi aliimarisha mamlaka yake baada ya kurekebisha katiba, na kumruhusu aliye madarakani kuwania muhula wa tatu. Mabadiliko hayo pia yalirekebisha urefu wa mihula ya urais kutoka miaka minne hadi sita, jambo ambalo litamfanya El-Sissi asalie madarakani hadi 2030 iwapo atashinda.

Licha ya el-Sissi kutoa wito kwa "Wamisri kushuhudia tukio hili la kidemokrasia, na kuchagua mtu anayefaa kwa jukumu hilo," katika kongamano mwishoni mwa wiki iliyopita, Kaldas anachukulia kura inayokuja kama "ukumbi wa michezo wa kuigiza."

"Kama kungekuwa na uchaguzi wenye ushindani, El-Sissi angekuwa hatarini sana," alisema. "Kutoridhika kwa umma na uongozi, kuzorota kwa uchumi, na hali ya maisha ya Wamisri wengi imeshuka kwa muda wa uongozi wa el-Sissi."

Hali mbaya ya kifedha ya Misri

Misri imekumbwa na mzozo wa kiuchumi kwa miaka mingi, na vita vya Urusi nchini Ukraine vimezidisha hali ya kifedha ya nchi hiyo inayoagiza ngano - bei ya vyakula imepanda kwa karibu asilimia 72 katika mwaka uliopita.

Kulingana na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), ukuaji wa Pato la Taifa la Misri unatabiriwa kuwa asilimia 3.7 tu mwaka 2023, baada ya ukuaji wa asilimia 6.7 mwaka 2022. Nchi hiyo pia inakabiliana na mfumuko mkubwa wa bei wa asilimia 39, na ushukaji wa asilimia 50 katika thamani ya Pauni ya Misri dhidi ya Dola ya Marekani tangu Februari 2022, kulingana na Wakala Mkuu wa Uhamasishaji na Takwimu wa Misri.

vita vya Ukraine -  Bei ya bidhaa imepanda sana nchini Misri.
Bei ya juu ya bidhaa iliyosababishwa na vita vya Urusi nchini Ukraine imepunguza uwezo wa watu kunua nchini Misri.Picha: KHALED DESOUKI/AFP

Misri ilitia saini mkataba wa dola bilioni 3 (€2.85 bilioni) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) mwezi Desemba 2022. Hata hivyo, imepokea tu dola milioni 347 za mkopo huo kwa sababu taifa hilo bado halijatekeleza makato ya bajeti yanayohitajika na mageuzi. Wakati huo huo, akiba ya fedha za kigeni nchini inakaribia kuisha. Kwa kuzingatia takwimu hizi, maoni machache katika hotuba ya kampeni ya el-Sissi wikendi iliyopita yalisababisha ghadhabu.

Soma pia: Maoni: Wamisri hawana cha kuchagua

“Kama gharama ya maendeleo na ustawi wa taifa ni njaa na kiu, tusile wala kunywa,” alisema. Katika kujibu, Altantawy alichapisha kwenye X, ambayo zamani ilikuwa Twitter, kwamba "Wamisri walikufa njaa wakati wa utawala wako kwa sababu ya uongozi wako."

Washirika wa kimataifa wa Misri pia wameanza kutoa ukosoaji zaidi na matakwa. Kwa mfano, nchi za Ghuba, ambazo kwa muda mrefu zimeisaidia Misri kifedha bila masharti, "zimeweka wazi kabisa, hadharani na kwa faragha, kwamba haziridhiki na jinsi nchi hiyo inavyoendeshwa," Kaldas aliiambia DW.

'Wapinzani wa kisiasa wamenyamazishwa'

Misri, hata hivyo, haichunguzwi tu kiuchumi lakini pia juu ya rekodi yake mbaya ya haki za binadamu. Mashirika ya haki za binadamu kwa muda mrefu yamekadiria kuwa wafungwa 65,000 hadi 70,000 wa kisiasa wanazuiliwa kabla ya kesi zao au baada ya kesi zisizo za haki katika magereza ya Misri. Katika maandalizi ya uchaguzi wa rais, ukandamizaji huu umeongezeka kwa mara nyingine tena.

Mapema wiki hii, shirika la haki za binadamu la Redress, na mashirika kadhaa yasiyo ya kiserikali ya Misri yalihitimisha katika uchambuzi wa kisheria kwamba matumizi ya mateso na mamlaka ya Misri yalikuwa yameenea sana na ya utaratibu kiasi kwamba yalifikia uhalifu dhidi ya ubinadamu chini ya sheria za kimataifa. Mashirika yasiyo ya kiserikali yaliwasilisha ripoti hiyo kwa Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Mateso kabla ya mapitio yake ya rekodi ya Misri mwezi Novemba.

Al-Sissi ataka suluhisho wakimbizi Afrika

Soma pia: Ufaransa yashutumiwa kusaidia ukandamizaji wa al-Sissi

"Wapinzani wa kisiasa wamenyamazishwa kwa kuwekwa jela, mashirika ya kiraia yana mipaka kwa kufanya utoaji wa leseni kuwa mgumu sana, na kuandaa [maandamano] imekuwa ngumu sana, kwani nafasi ya kisiasa imemomonyoka katika miaka 10 iliyopita," Lina Attalah, mhariri mkuu wa Mada Masr, aliiambia DW.

Hilo ndilo linalofanya maandamano ya nchini nzima mapema wiki hii kuwa ya kuvutia. Mikutano kadhaa iliyofadhiliwa na serikali ya kusherehekea tangazo la kugombea el-Sissi iligeuka kuwa maandamano dhidi ya serikali, lakini ilitupiliwa mbali mara moja kama mikusanyiko ya sanaa na mamlaka, kulingana na shirika la habari la Ujerumani dpa.

Video nyingi kwenye mitandao ya kijamii, zilizothibitishwa kuwa sahihi na wanaharakati wa Misri, zilionyesha watu wakipiga kelele: "Watu wanatoa wito wa kuanguka kwa utawala."