1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la dunia 2010

27 Machi 2009

Ujerumani ina miadi leo na Liechtenstein.Kamerun na Togo.

https://p.dw.com/p/HKqC
Lukas PodolskiPicha: AP

Mwishoni mwa wiki hiii ,Ligi nyingi zimesimama tena takriban katika kanda zote za FIFA-shirikisho la dimba ulimwenguni.Zinatoa nafasi kwa timu za Taifa kuteremka viwanjani kuania tiketi zao kwa Kombe lijalo la dunia 2010 nchini Afrika Kusini: Kanda ya Afrika pia inateremka uwanjani huku simba wa nyika-Kamerun na Super Eagles-Nigeria, wakitaka kufuta madhambi ya kombe lililopita la dunia 2006 walipokosa kuja Ujerumani.

Ujerumani ina miadi leo mjini Leipzig na chipukizi Liechtenstein kabla jumatano ijayo, haikutolewa jasho na Wales.Kuhakikisha katika mapambano hayo 2 Ujerumani haitelezi katika njia yake kuelekea Afrika Kusini, kocha Joachim Loew, amemuita tena uwanjani mshambulizi wa Bayern Munich,Lukas Podolski.Kocha Loew sio tu anazihitaji pointi 3 leo ili kushika usukani wa kundi lake la 4,bali anaitaka timu yake kuonesha mchezo bora zaidi kufuatia misukosuko iliopata ya kushindwa mara 2 zilizopita-kwanza na England-Uingereza na halafu na Norway.

Ujerumani tangu kulazwa na Spian katika finali ya Kombe la UIaya 2008,ufa umeimngia katika timu hii na hii imeongoza katika mpapurano baina ya wachezaji na hata kati yao na kocha wao Joachim Loew.Hasa nahodha Michael Ballack amekuwa shina la mabishano hayo.Kwa mpambano wa leo,Ballack amenuwia kuona jahazi lake haliendi mrama na linaelea hadi hapo oktoba na Urusi ambayo haitakua mboga mchicha kama Liechtenstein jioni hii.

Usoni Ujerumani haina matatizo makubwa leo kinyume na katika ngome yake ambako kipa wake Adler ameumia.Kwa kuumia Miroslav Klose, Ujerunai itamtegemea Podolski kupiga hodi mara kwa mara katika lango la Liechtenstein na keshokutwa la wales hadi kuitikiwa.Atasaidiwa na washambulizi 2 wa Bayer Leverkusen: Patrick helmes na Stefan Kiessling.

Mabingwa wa dunia Itali wakiongozwa tena na kocha wao aliewatawaza mabingwa wa dunia hapa ujerumani 2006,Marcello Lippi,hadiriki kosa jengine leo ikiwa Squad Azzurri -itetee taji lake huko Afrika Kusini,mwakani.Mabingwa hawa wa dunia, wanalitoa maanani pigo la mabao 2:0 mwezi uliopita kutoka kwa mabingwa wa Amerika kusini-Brazil .

Katika kanda ya Afrika, kwa mashabiki wa ndovu 2 wa dimba barani Afrika-simba wa nyika-Kamerun na Super Eagles-Nigeria, ilikuwa kuvunjwa moyo kwa kukosa kushiriki katika kombe lililopita la dunia 2006. Mara hii likichezwa nyumbani Afrika ,simba wa nyika- Kamerun na Nigeria, wanadai lazima wawepo.

Hatahivyo, Nigeria ina kibarua kigumu kundi B,kwani sio tu itawapasa kutamba mbele ya Harambee Stars (Kenya) na Msumbiji,wanahitaji pia kuwapiku Watunisia wanaocheza na Harambee Stars.Tunisia imecheza katika mashindano 3 yaliopita ya Kombe la dunia na hizo ni salamu ambazo haziwezi kupuuzwa.

Simba wa nyika Kamerun ,ilikuwa msiba kwao kutonguruma hapa Ujerumani 2006 na ili kurekebisha madhambi hayo, kocha wao mjerumani Otto Pfister amefunga safari na simba wake leo hadi Lome kwa changamoto ya kundi B na Togo.Togo ndio iliocheza kombe lililopita la dunia na kuiacha Kamerun nyuma.Kwani, laiti mwakkwaju wa Pierre Wome, beki wa sasa wa FC Cologne katika Bundesliga, ungenasa kimiyani, ingelikua kamerun ingekuja Ujerumani na sio Tembo wa Corte d-Iviore.

Katika kundi C,madume 2 wanaotazamiwa kwenda Afrika kusini kwa Kombe la Dunia-Misri,mabingwa wa Afrika na Zambia-(Chipolopolo) wanapambana mjini Cairo.Rwanda iko nyumbani ikiikaribisha Algeria.Washindi 5 wa makundi haya mbali mbali kanda ya Afrika, watajiunga na wenyeji Bafana bafana-au Afrika Kusini kuchangia timu 6 za Afrika kwa Kombe la dunia 2006,wakati timu 3 za usoni kabisa kutoka m akundi hayo,tutaziona uwanujani nchi jirani Angola kuania kujaribu kuwavua taji mafiraouni-Misri.

Muandishi: Ramadhan Ali

Mhariri: A.Liongo