1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wasserforum Istanbul

Oumilkher Hamidou16 Machi 2009

Maji ni tunu na adimu lakini yanatumiwa ovyo ovyo wanalalamika washirika katika kongamano la Istanbul nchini Uturuki

https://p.dw.com/p/HDNu
Mwanamfalme Albert wa Monaco (kati) akizungumza na rais ASbdullah Gül wa Uturuki (kulia) na rais Jalal Talabani wa Irak(kushoto) katika kongamano la maji mjini IstanbulPicha: AP


Kongamano la tano la kimataifa kuhusu maji limefunguliwa leo mjini Istanbul nchini Uturuki. Kongamano hilo kubwa la aina yake litakaloendelea hadi jumapili ijayo  linajadili masuala, miongoni mwa mengineyo, kuhusu namna ya kutumia mali ghafi hiyo ya tunu na yenye thamani hadi kufikia vizazi vijavyo.


Vyombo vya habari vya Uturuki vinazungumzia juu ya washiriki 20 elfu wa kongamano hilo, wakiwemo viongozi wa taifa na serikali kutoka zaidi ya nchi 100.


Kila mtu anatambua kwamba maji ambayo yamekua haba yanabidi kuhifadhiwa.Kwa sababu shehena ya maji safi ya kunywa kutoka ardhini imeingia hatarini kutokana na mitindo isiyofaa na iliyokithiri ya kunyunyizia maji pamoja pia na matumizi mabaya ya maji hasa katika nchi za magharibi. Maji yanayotumiwa na mtu mmoja  na kwa mwaka, kwa mfano, nchini Marekani na katika nchi za Ulaya yanapindukia mita elfu kumi za ujazo -kiwango ambacho ni kikubwa mara sabaa kikilinganishwa na kiwango cha maji anachotumia mkaazi mmoja wa Syria kwa mwaka ambacho ni cha mita 1450 za mjazo.Katibu mkuu wa kongamano hili la tano la kimataifa kuhusu maji, Proffesor Oktay Tabasaran anasisitiza kwa kusema:


"Kwa mtazamo wa muda mrefu, maji ya kunywa ni kitu adimu.Watu bilioni mbili mbili kote ulimwenguni hawapati maji safi ya kutosha.Kila mwaka watu milioni 200 wanashikwa na maradhi kutokana na kutumia maji machafu na kwa bahati mbaya watu karibu milioni mbili wanafariki dunia kwaajili hiyo."


Hata kama thuluthi mbili ya dunia yetu imejaa maji, asili mia 97 nukta tano ya maji hayo ni ya chumvi. Na asili mia 70 ya maji matamu yaliyosalia yamegeuka theluji na kuganda katika ncha za dunia yetu. Asili mia 30 zilizosalia zinatumika kurutubisha ardhi au kama shehena ya maji ya chini ya ardhi.


Kutokana na kuzidi kuongezeka idadi ya wakaazi wa dunia kwa karibu watu milioni 80 kwa mwaka,vikomo hivyo vinazidi kuwa tatizo, seuze, na hapa imedhihirika hata mjini Istanbul, maoni ya jinsi ya kuhifadhi maji na kuyagawa kwa njia za usawa yanatofautiana. Ndio maana wakosoaji wa kongamano hili litakalogharimu Euro  milioni 17 na nusu wameandaa mkutano mbadala. Kwa sababau wanahisi washiriki wenyewe wa kongamano hilo ndio sehemu ya tatizo. Wanawakosoa kutaka kuutumia mzozo wa maji kibiashara tuu.


Mwandishi:  Ulrich Pick/ Hamidou Oummilkheir ZR

Mhariri:  Miraji Othman