1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

London: Polisi wagundua bomu la pili London.

30 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBn8
Polisi wa Uingereza wamesema wamegundua bomu la pili lililotegwa kwenye gari katikati ya jiji la London saa chache baada ya kutegua bomu jengine sawa na hilo nje ya klabu moja ya usiku jijini humo.

Mkuu wa kikosi cha polisi wa kukabiliana na ugaidi jijini London, Peter Clarke amesema magari yote mawili yana uhusiano.

Polisi hapo awali walisema bomu la kwanza lilikuwa na uzito wa kuweza kusababisha maafa makubwa.

Waziri wa mambo ya ndani wa Uingereza Bi Jacqui Smith amewataka wakazi kuendelea kuwa waangalifu.

Waziri Jacqui Smith amewashukuru wataalamu wa mabomu kwa kazi yao nzuri. Amesema amekutana na baraza la mawaziri wenzake na pia waziri mkuu kuwapasha hali ilivyo.

Bi Jacqui Smith asema ni vizuri polisi wapewe fursa ya kufanya upelelezi wao bila ya watu kueneza uvumi usiokuwa na msingi.

Mashambulio hayo yametibuliwa siku mbili baada ya Gordon Brown kukabidhiwa rasmi wadhifa wa Waziri Mkuu wa Uingereza, na pia siku chache kabla ya Julai tarehe saba ambayo ni siku ya ukumbusho wa miaka miwili tangu mashambulio ya mwaka 2005 yaliyolenga mfumo wa usafiri wa London.