1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel asisitiza kuwepo kwa taifa la Kipalestina

1 Februari 2011

Wakati hali ya upinzani dhidi ya Rais Hosni Mubarak ikizidi huko, Misri, Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ameitaka Israel kuchukua hatua mujarab za kuhakikisha kuendelea kwa mazungumzo ya amani ya Mashariki ya Kati.

https://p.dw.com/p/108CH
Kansela Angela Merkel na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanjahu mjini Jerusalem.Picha: dapd

Alisema hayo katika mkutano wake na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu mjini Jerusalem, kuhusiana na hali ilivyo hivi sasa kwenye eneo hilo.

Kansela Merkel na karibu nusu nzima ya baraza lake la mawaziri yuko ziarani nchini Israel.

Kansela Merkel amesema ni muhimu kuchukuliwa kwa hatua za haraka za kuendeleza mazungumzo ya amani ya Mashariki ya kati.

Amwambia Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu wazi wazi , kwamba kuwepo kwa taifa la kipalestina ndiyo suluhisho la mzozo wa eneo hilo.

Weltwirtschaftsforum Davos Bundeskanzlerin Angela Merkel
Kansela Angela MerkelPicha: AP

´´Mtizamo wangu ni kwamba, kile ambacho tunachokitaja, kimsingi katika hali hii inayoendelea ni kuwepo kwa mazungumzo ya amani.Tunataka kuwepo kwa mataifa mawili kama suluhisho la mzozo huo.Ujerumani imekuwa mara zote ikisema kuwepo kwa taifa la kiyahudi na taifa la kipalestina.Na bilashaka nimekwishasema kuwa, kwa mtizamo wangu jambo hili ni lazima lifanyike haraka iwezekanavyo´´ alisisitiza

Matamshi hayo ya Kensela Merkel yameongeza mbinyo wa kurejea kwenye mazungumzo ya ana kwa ana kati ya Israel na mamlaka ya Wapalestina.Zaidi ya hayo Kansela Merkel akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, alirudia kauli yake ya mara kadhaa kutaka kusitishwa kwa ujenzi wa makaazi ya walowezi katika maeneo ya wapalestina akisema hatua hiyo ni muhimu.

Kwa Upande wake Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alimshukuru Kansela Merkel pamoja na baraza lake la mawaziri kwa kuizuru Israel kwa ajili ya majadiliano kati ya serikali za nchi hizo mbili.Suala hilo la ujenzi wa makaazi ya walowezi katika maeneo ya wapalestina limekuwa suala nyeti katika kufikiwa kwa makubaliano ya amani katika mzozo wa zaidi ya miaka 50 sasa na hakujapatikana suluhisho lake.

Kuhusiana na hali nchini Misri,Kansela Merkel ambaye hapo siku ya Jumapili alizungumza kwa njia ya simu na Rais Hosni Mubarak, na kutaka kuchukuliwa kwa hatua za kidiplomasia kutegemeana na hali itakavyokuwa siku zijazo, alisema ni muhimu kwamba kunakuwepo na majadiliano ya amani na kwamba maoni na haki ya uhuru wa kuandanama vinaendelea kuheshimiwa.

´´Majadiliano haya muhimu na kwa mtizamo wangu vilevile iwapo kwamba kutakuwepo na mgomo mkubwa, basi vifanyike kwa utulivu na amani, kuwafanya waweze kufanya mabadiliko ya sheria.Rais amekwishatangaza kufanyika kwa mabadiliko, lakini ni wazi, bado hayajaturidhisha kutimiza kile kinacholalamikiwa´´alisema

Israel Palästinenser Gaza Ministerpräsident Benjamin Netanyahu
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin NetanyahuPicha: AP

Naye Bwana Netanyahu amesema ana wasiwasi na hali inayoweza kutokea nchini Misri, kwamba inatokana na kutokuwepo kwa muundo wa kidemokrasia ambao ni muhimu katika hatua za kidemokrasia zinazotaka kuchukuliwa.

Ametoa mfano wa Iran katika mapindinduzi ya kiislam ya mwaka 1979 jinsi ambavyo utawala wa uonevu wa Shah ulivyoondolewa madarakani na utawala wenye kufuata mfumo wa kiislam.Kwa kile kinachoendelea hivi sasa nchini Misri, Bwana Netanyahu anaona ni kitisho kwa amani.

Hata hivyo amesema Israel ina matumaini amani na utulivu vitadumishwa, akigusia mkataba wa amani wa mwaka 1979 uliyotiwa saini kati ya Israel na Misri.

Mwandishi:Clemens Verenkotte/Aboubakary Liongo.

Mhariri:Abdul Mtullya.