1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa watoa wito wa kusadia Pembe ya Afrika

Admin.WagnerD21 Julai 2011

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ametoa wito kwa nchi wahisani kusaidia kiasi cha euro bilioni 1.6 kwa haraka ili kuweza kusaidia majimbo mawili nchini Somalia yaliyothibitishwa kukumbwa na balaa la njaa.

https://p.dw.com/p/120ja
Wanawake wakiwa kati foleni ya kupata chakula cha msaada SomaliaPicha: dapd

Katibu Mkuu Ban Ki-moon amesema kiasi ya watu milioni 3.7 hivi sasa wanakabiliwa na janga hilo sio tu Somalia peke yake bali hadi katika maeneo ya nchi jirani. Somalia kama nchi iliyokabiliwa na migogoro kwa zaidi ya miaka 20 sasa na kuonekana kama taifa lisilofanikiwa duniani limeathirika sana na janga hilo.

Lakini maeneo mengine ambayo hali imekuwa mbaya yapo nchini Kenya, Uganda, Ethiopia na Djibouti.

Tathimini ya ujumla ambayo imetolewa mara kadhaa katika vyombo vya habari inaeleza kuwa kiasi ya watu milioni 12,wanakabiliwa na janga hilo ambalo halijawahi kutoikea katika kipindi cha miaka sitini.

Felix Musenye ni Meneja wa Shirika la Kijerumani la Msalaba Mwekundu linaloshughulikia majanga katika eneo la Afrika Mashariki lakini kwa hivi sasa limejikita Kenya na Somalia. Kwanza anaelezea mchango wa shirika hilo kwa hivi sasa kufuatia hali ilivyojitokeza.

Valerie Amos UN Nothilfekoordinatorin in Somalia
Mwanamke aliyekimbia makazi yake nchini SomaliaPicha: AP

Kwa Mujibu wa Musenye Wajerumani wametenga kiasi cha euro laki tatu katika kuwanusuru wahanga wa balaa la njaa. Hata hivyo kiasi hicho cha pesa kimeonekana kuwa hakitoshi na hivyo kuhimiza wafadhili zaidi kuchangia kuwanusuru raia wengi wanaokabiliwa na balaa hilo.

Kwa upande wao shirika la kimataifa la misaada ya kiutu la Oxam limesema nchi za Umoja wa Ulaya zimeshindwa kutoa msaada wa kukabiliana na balaa la njaa katika eneo la Pembe ya Afrika.

Lawama hizo zinatolewa wakati Umoja wa Mataifa wametangaza kuwepo kwa balaa la njaa katika maeneo ya kusini mwa Somalia. Katika ripoti yake Oxfam, inaeleza kuna upungufu wa dola bilioni 1 katika kufanikisha misaada ya kiutu katika ukanda huo, ikijumuisha dola milioni 296 kwa ajili ya Somalia.

Mkuu wa Oxfam kwa upande wa ofisi ya Umoja wa Ulaya, Natalia Alonso amesema nchi za ulaya zimekuwa zikichukua hatua za taratibu mno kukabiliana na janga hilo.

Mpaka sasa Uingereza imeahidi dola milioni 145, Uhispania dola milioni10, Ujerumani dola milioni 8.5, na umoja wa Ulaya dola milioni 5.7 huku misaada zaidi ikitarajiwa.

Kwa upande wao Umoja wa Mataifa umesema unahitajika kiasi cha dola bilioni 7.9 kwa mwaka huu peke yake ili kuweza kukabiliana misaada ya kiutu katika nchi za Afrika na Asia.

Mwandishi: Sudi Mnette
Mhariri: Abdul-Rahman