1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kampuni la Chrysler lafilisika

Oumilkher Hamidou1 Mei 2009

"Muflis ni njia mojawapo ya kujirekebisha",anasema rais Obama

https://p.dw.com/p/Hi4B
Rais Obama atangaza kufilisika ChryslerPicha: AP

Kampuni la magari la Marekani Chrysler limejitangaza muflis na linadhamiria kushirikiana na kampuni la magari la kitaliana Fiat.

Alikua mwenyewe rais barack Obama aliyetangaza habari hizo jana.Kampuni hilo la magari la Marekani Chrysler limefikia hali hiyo baada ya mazungumzo ya awali pamoja na kundi la waiya kushindwa hapo awali.

Rais Barack Obama anasema kwa kujitangaza muflis,haimaanishi kwamba Chrysler halina tena maana:

"Hii si dalili ya udhaifu,bali ni hatua inayoonyesha kwamba juhudi zaidi zinaendelezwa ili kuliimarisha kampuni la Chrysler."

Kifungu nambari 11 cha sheria za Marekani,kinasema kujitangaza muflisi haimaanishi kvunjika kampuni.Kinyume kabisa,kampuni linajipatia fursa ya kusaka njia nyengine za kujiimarisha.Hata hivyo serikali ya Marekani ilitaraji kuepukana na hali hiyo.Waiya walishauriwa wakubali kupokea dala miliadi 2.25 kufidia deni linalofikia dala miliadi 6.9.Wengi wao walikubali.Rais Barack Obama alilitaja kampuni la magari la Ujerumani Daimler lililoridhia kutodai sehemu yake na kujiunga na mpango wa malipo ya uzeeni,uamuzi ambao unalipunguzia gharama kampuni la Chrysler.

Hata hivyo baadhi ya waiya hawajakubaliana na shauri hilo na muda uliowekwa na serikali ukamalizika jana-ndio maana Chrysler likajitangaza muflis.Hivi sasa litakua jukumu la mahakama kuamua waia gani wanastahiki kulipwa fedha nyingi zaidi kuliko zile zilizopendekezwa na serikali ya Marekani.

Serikali ya Marekani inataraji hali ya muflis haitopindukia kaati ya siku 30 mpaka 60.

Wakati huo huo rais Barack Obama amezungumzia juu ya makubaliano ya ushirikiano yaliyofikiwa kati ya Chrysler na kampuni la magari la Italy Fiat.Makubaliano hayo, amesema rais Obama yatasaidia kuzinusuru nafasi zaidi ya 30 elfu za kazi pamoja na maelfu ya nafasi nyengine katika makampuni yanayotengeneza vipuri,wauza magari na makampuni mengineyo.

Kampuni la Fiat litakua na nafasi ya kumuiliki asili mia 51 ya hisa,mikopo yote itakapolipwa.

"Ni mshirika atakaelipatia kampuni la Chrysler,sio tuu nafasi ya kujinusuru bali pia kujiimarisha na kuibuka kua sekta muhimu ya magari ulimwenguni",amesisitiza rais Barack Obama.

Kwa pamoja makampuni hayo yanaweza kuuza magari milioni nne na laki 16 kwa mwaka,kiwango ambacho ni sawa na kile cha magari yanayouzwa na kampuni la Hyndai,yakitanguliwa na Toyota,General Motors,Volkswagen na Ford.

Kabla ya Fiat kumiliki sehemu kubwa ya hisa,shirika la wafanyakazi wa viwanda vya magari UAW ndilo litakalomiliki sehemu kubwa ya hisa.

Vyombo vya habari vya Italy vinasifu makubaliano kati ya Fiat na Chrysler.Kampuni hilo la kitaliana linasema linataka kufikia pia makubaliano pamoja na kampuni la magari la General Motors.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Abdul Rahman