1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

AFCON 2013; Nigeria kutoroka na kombe?

10 Februari 2013

Nigeria inaonekana karatasini inaweza kutoroka na taji la ubingwa wa kombe la mataifa ya Afrika leo jioni(10.02.2013)ikipata ushindi wake wa tatu katika mashindano haya katika uwanja wa soccer City mjini Johannesburg.

https://p.dw.com/p/17bZG
epa03570880 Nigeria players celebrate after Elderson Echiejile (L) scored the first of three first half goals during the semi-final match in the Africa Cup of Nations between Mali and Nigeria played at The Moses Mabhida Stadium, Durban, South Africa, 06 February 2013. EPA/KIM LUDBROOK +++(c) dpa - Bildfunk+++
Wachezaji wa nigeria wakifurahia baoPicha: picture-alliance/dpa

Lakini uwezekano kwa Burkina faso kuonyesha maajabu katika fainali hiyo hauwezi kupuuzwa.

Vikosi vyote viwili vilianza kampeni yake kwa matumaini finyu lakini viliweza kusonga mbele hadi fainali katika mashindano ambayo yalikumbwa na maajabu kadha.

Nigeria , licha ya kuwa kigogo katika soka ya Afrika, iliweka wazi kuwa inaona mashindano haya nchini Afrika kusini kama fursa ya kutayarisha kikosi kipya, wakati Burkina Faso ilionekana wakati wote kuwa ni wasindikizaji tu.

Pamoja na hayo timu zote hizo zimeweza kuvuka vikwazo kadha na kufikia fainali , ambapo Burkina faso inakuwa mara yake ya kwanza kufikia kiwango hicho.

Ghana's Isaac Vorsah, right, defends against Burkina Faso's Aristide Bance, left, during their African Cup of Nations semifinal soccer match at Mbombela Stadium in Nelspruit, South Africa, Wednesday Feb. 6, 2013. (AP Photo/Themba Hadebe)
Mpambano kati ya Ghana na Burkina FasoPicha: picture alliance/AP Photo

Ikiwa katika nafasi ya 92 katika orodha ya timu bora duniani kwa mujibu wa shirikisho la kandanda ulimwenguni FIFA, Burkina Faso imepindukia matarajio ya ndoto yao kwanza kwa kushika nafasi ya kwanza katika kundi lao, na kisha kuipiga mwereka Togo baada ya muda wa nyongeza katika robo fainali na kuiweka kando Ghana kwa mikwaju ya penalti katika mpambano wa kuvutia wa nusu fainali Jumatano iliyopita.

Burkinabe kubadili uwanja

Michezo yao yote mitano , ikiwa ni pamoja na sare ya bao 1-1 dhidi ya Nigeria katika siku ya tatu ya mashindano hayo ilichezwa katika uwanja unaoonekana kuwa na mchanga zaidi ya majani wa Nelspruit, lakini sasa watakabiliana katika mchezo wao wa kwanza katika uwanja ulioko katika eneo la karibu mita 1,750 juu ya usawa wa bahari mjini Johannesburg.

Nigeria ambayo imecheza michezo yake miwili mjini Rustenburg katika eneo la mita 1,100 juu ya usawa wa mahari, inacheza katika fainali yake ya saba ya kombe la mataifa ya Afrika katika muda wa miaka 13.

Licha ya kuwa taifa hilo lenye wakaazi wengi katika bara la Afrika na nchi ambayo mara kwa mara hutoa vijana wenye vipaji vya uchezaji wa soka kwenda kuchezea nje ya nchi hiyo katika vilabu mbali mbali duniani , wameweza kushinda mashindano hayo mwaka 1980 na 1994 tu.

Kocha Stephen Keshi alikuwa nahodha wa Green Eagles, mara ya mwisho walipolinyakua kombe hilo, na iwapo Nigeria itafanikiwa kulitwaa kombe hilo mara hii, atakuwa mtu wa pili kufanya hivyo kama mchezaji na kocha, akifuata nyayo za Mahmoud al-Gohari wa Misri.

Mali yala shaba

Wakati huo huo Mali imerudia kile ilichofanya mwaka jana katika mashindano haya , kwa kutwaa medali ya shaba, baada ya kuishinda Ghana kwa mabao 3-1.

Malian players celebrate with their bronze medal at the end of the 2013 African Cup of Nations third place final football match Mali vs Ghana, on February 9, 2013 in Port Elizabeth. Mali won 3 to 1. AFP PHOTO / ISSOUF SANOGO (Photo credit should read ISSOUF SANOGO/AFP/Getty Images)
Mali yanyakua medali ya shabaPicha: Getty Images

Mwaka jana Mali iliishinda Ghana kwa mabao 2-0 katika mchezo huo wa kutafuta mshindi wa tatu. Wachezaji wa Mali waliingia katika mashindano ya mwaka huu wakisema kuwa wanataka kuleta furaha kwa mashabiki nyumbani kwao ambao wanakabiliwa na msukosuko wa kisiasa na hali isoyokuwa thabiti ya kiusalama.

"Nimefurahi na ninajisikia fahari . Wachezaji wamejituma kwa moyo wao wote na kuleta medali ya shaba", kocha wa Mali Patrice Carteron amesema. " Kwa taifa kama Mali , haya ni matokeo mazuri sana". Kipigo ilichopata Ghana kimeongeza zaidi hali ya kukatisha tamaa, timu ambayo imefikia nusu fainali mara nne zilizopita lakini inaondoka tena bila ya taji.

PORT ELIZABETH, SOUTH AFRICA - FEBRUARY 09: Keita Seydou of Mali celebrates scoring the 2nd goal during the 2013 Africa Cup of Nations Third Place Play-Off match between Mali and Ghana on February 9, 2013 in Port Elizabeth, South Africa. (Photo by Ian Walton/Getty Images)
Nahodha wa Mali Seydou Keita akishangiria bao dhidi ya GhanaPicha: Getty Images

Ghana iliambulia kushiriki katika kuwania nafasi ya tatu baada ya kushindwa katika mpambano wa nusu fainali na Burkina Faso katika mikwaju ya penalti. Black Stars walishinda mara ya mwisho ubingwa wake wa nne mwaka 1982.

Mwandishi : Sekione Kitojo / ape / rtre

Mhariri: Amina Abubakar