1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiAfrika Kusini

Afrika Kusini yazuia watoto 400 wa Zimbabwe kusafirishwa

Angela Mdungu
4 Desemba 2023

Maafisa wa usimamizi wa mipaka nchini Afrika ya Kusini wamesema wamefanikiwa kuyakamata mabasi takribani 40 yaliyowabeba zaidi ya watoto 400 waliokuwa wakisafiri bila ya wazazi wala walezi.

https://p.dw.com/p/4Zlao
Mtoto
Biashara haramu ya kuwasafirisha watoto Picha: Pond5/Imago Images

Mabasi hayo yamekamatwa wakati wa operesheni maalumu ya kupambana na usafirishaji haramu wa binadamu. Kamishna wa shirika la usimamizi wa mipaka la Afrika ya Kusini Mike Masiapato, amethibitisha kuwa Jumamosi usiku waliwapata watoto 443 wenye chini ya umri wa miaka 8 wakisafiri peke yao katika mabasi yaliyokuwa yakitokea Zimbabwe.

Amesema maafisa wa polisi waliyasimamisha na kuyapekua mabasi 42 na kuwakuta watoto hao waliokuwa wakisafirishwa kinyume cha sheria kuingia nchini humo. Mabasi hayo yaliyokamatwa hata hivyo yaliamriwa kurejea Zimbabwe.

Mtoto wa Afrika Kusini
Mtoto wa Afrika Kusini akiwa amebeba bango lenye ujumbe wa kupinga usafirishaji haramu watotoPicha: NIC BOTHMA/EPA/dpa/picture alliance

Kutokana na tukio hilo, mashirika yanayowawakilisha raia wa kigeni waishio Afrika ya Kusini yamesema kuna uwezekano kuwa watoto waliokuwa kwenye mabasi hayo yaliyokamatwa walikuwa wakipelekwa kuwatembelea wazazi wao wanaoishi nchini humo wakati huu wa msimu wa  kuelekea mwisho wa mwaka, suala ambalo mwenyekiti wa jukwaa , la Africa  Diaspora Ngqabutho Mabhena, linalowakilisha raia wa kigeni wanaoishi Afrika Kusini, amesema kuwa shirika lake linaamini ni la kawaida wakati wa majira ya mwisho wa mwaka.

Soma hapa: Tanzania lawamani kwa kutozuia utumikishwaji wa watoto

Hata hivyo Mabhena amesema wamekuwa wakiwaasa wazazi hao raia wa Zimbabwe kuhakikisha wanapopanga safari za kuwaalika watoto wao Afrika ya Kusini wanakuwa na vibali vyote vinavyohitajika. Ameongeza kuwa ni uzembe kuwaacha watoto wasafiri na watu wasio wajua na bila ya kuwa na pasi za kusafiria.

Usafirishaji haramu wa binaadamu watishia watoto wa Afrika

Baadhi ya Wazimbabwe wanaishi Afrika ya Kusini wengi wao kinyume cha sheria baada ya kuhamia katika taifa hilo jirani ndani ya miaka 15 iliyopita wakikimbia hali ngumu ya uchumi ya Zimbabwe.

Soma zaidi: Mtu na mkewe raia wa Marekani washtakiwa Uganda

Kulingana na shirika la habari la AP kuna, karibu raia 178,000 wa Zimbabwe wanafanya kazi na kuishi Afrika ya kusini kisheria chini ya kibali maalumu kinacho wapa msamaha. Licha ya hilo, sensa ya Afrika ya Kusini ya mwaka 2022 ilionesha kwamba kuwa zaidi ya Wazimbabwe milioni moja nchini humo. Badhi ya watu wanakadiria kuwa idadi ya raia hao wa Zimbabwe ni watu milioni tatu katika taifa hilo.

Afrika ya Kusini moja ya nchi zenye uchumi mkubwa zaidi katika bara la Afrika iliunda kikosi kipya cha kusimamia mipaka mnamo mwezi Oktoba. Madhumuni ya kuundwa kwa kikosi hicho ni kukabiliana na uhamiaji haramu kutoka Zimbabwe pamoja na mataifa mengine.