1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afya ya Kansela wa Ujerumani Angela Merkel yazua wasiwasi

11 Julai 2019

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wameandika kuhusu wasiwasi juu ya afya ya Kansela Angela Merkel baada ya kuonekana hadharani akitetemeka tena na sakata la Chama cha AfD baada ya kuvunja moja ya sheria za uchaguzi

https://p.dw.com/p/3Lube
Angela Merkel
Picha: Reuters/F. Bensch

Wengi wa wahariri wakiwemo wa magazeti ya Schwäbische Zeitung na Oberhessische Presse wameandika juu ya afya ya Kansela Angela Merkel wa Ujerumani. Mhariri wa gazeti la Neue Osnabrücker anaandika kutetemeka kwa Kansela kunaleta hofu si tu kwa Ujerumani bali duniani kote. Anaendelea kusema, afya ni jambo binafsi kwa kiongozi wa serikali, lakini hilo ni kwa kiasi fulani pekee. Mhariri wa gazeti hili ameandika baada ya Kansela kuonekana akitetemeka kwa mara ya tatu ndani ya wiki chache mbele ya kamera, maelezo yaliyowahi kutolewa awali hayatoshi kuwaondoa watu wasiwasi na kwamba itakuwa vyema iwapo maelezo zaidi yatatolewa ili suala hili lisiwe la kisiasa.

Kusomwa hukumu ya Ali B juu ya tuhuma za mauaji

Baada ya hukumu iliyotolewa hapo jana 10.09.2019 kuhusu kijana mkimbizi Ali B, aliyekuwa akituhumiwa kumbaka na kisha kumuua binti Sussana aliyekuwa na umri wa miaka 14 mhariri wa gazeti la Wiesbadener Kurier anaeleza kuwa kila jambo sasa limekuwa wazi mbele ya sheria. Hukumu hiyo sio kwa nia ya kufurahisha watu bali watu walikuwa wakitegemea hukumu hiyo. Katika kuzingatia hukumu hiyo hiyo sehemu ya maoni ya mhariri wa gazeti la Frankfurter Rundschau inasema hatua hiyo haikuwa tu muhimu katika kuheshimu kumbukumbu ya binti Sussana, bali pia ni kutenda haki kwa mama wa binti huyo.

Kuhusu mtikisiko uliokikumba chama cha mrengo wa kulia cha AfD baada ya kuvunja moja ya kanuni za sheria ya uchaguzi unaovitaka vyama vya siasa kuwasilisha orodha moja pekee ya wagombea na badala yake kuwasilisha orodha mbili katika jimbo la Saxony, wahariri wa magazeti ya Passauer Neue Presse na Volksstimme wameandika pia  maoni yao. Gazeti la Passauer Neue Presse linaandika kilichotokea kwa AfD kwa sasa hakiwezi kuzuilika, kimeshatokea na kwamba kama chama mbadala cha Ujerumani kinataka kuonekana chenye umuhimu hakina budi kuchukua hatua za kuanza kujisafisha. Anamalizia kwa kusema AfD inahitaji  kuwa na mtazamo tofauti na ule wa mmoja wa wasemaji wake Björn Höcke, kwa kujitenga na mawazo ya kinazi.

 

dpae, inlandspresse