1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Al-Shabab wafurushwa mafichoni

12 Aprili 2012

Viogozi na askari wa miguu wa kundi la wanamgambo wa al-Shabab wanakimbia kutoka maficho yao katika eneo la milima ya Kaskazini-mashariki mwa Somalia.

https://p.dw.com/p/14c9b
Picha: AP

Hali ya mashinikizo makubwa ya kivita kutoka wanajeshi wa Uganda, Burundi, Ethiopia na Kenya ambapo wanamgambo hao walishambuliwa kupitia kaskazini mwa Safu ya Milima ya Galgala-Putland kwenye taifa lililojitenga la Somaliland, imewafurusha al-Shabab kutoka mafichoni mwao.

Waziri Mkuu wa Somalia Abdiweli Mohamed Ali amesema kwa sasa wanamgambo wa al-Shabab wameishiwa nguvu na wanakimbilia milima hii ya Galgala ambapo ni eneo lenye mandhari ngumu kwao.

Akizungumza na mwanahabari mmoja amesema, hivi sasa al-Shabab wanaweka makao yao mapya katika eneo la Putland baada ya shinikizo la ushirikiano wa pamoja baina majeshi ya Somalia na majeshi ya Umoja wa Afrika. Huku dalili za kushindwa kwa al-Shabab zilianza kuonekana mwanzoni mwa mwezi Februari baada ya kufurusha katika mji wa Baidoa ambao ni mji wa tatu kwa ukubwa.

Wakipitia kaskazini mwa Somalia wanamgambo hao waliingia katika mji wa Mogadishu ambao shughuli za kawaida kama vile biashara, michezo na sanaa zilizoanza kurejea, mlipuaji wa kujitolea mhanga alijilipua bomu juma lililopita katika ukumbi wa kimataifa wa maonyesho na kusababisha watu 10 kufariki huku lengo la mlipuaji huyo likiwa ni kumuua Waziri Mkuu wa Somalia.

Waziri Mkuu apona katika shambulio.

Waziri Mkuu Ali mara baada ya tukio hilo alisema kuwa alishuhudia gafla moto na moshi wenye harufu kali baada ya bomu hilo kulipuka yeye akiwa jukwaani akitazama watu. Anasema ni tukio la kutisha mno.Tukio kama hilo ni la kustajabisha kutokea lakini ndivyo ilivyotokea kukiwa na uzembe wa usalama.

Kiongozi huyo kutoka taifa hili ambalo halijatengemaa kwa amani anasema hawezi kuofia kuuwawa akiwa Waziri Mkuu bali maafisa wa usalama wanajukumu la kuzuia mashambulizi ya karibu na viongozi kama haya.

Mfanyabiashara Atom atuhumiwa kusafirisha silaha.

Kwa miaka kadhaa wapiganaji wanaongozwa na mfanyabishara na mwanajeshi wa zamani Mohamed Said Atom, wamekuwa wakipigana na Serikali ya Putland wakishambulia kutokea milimani. Kulingana na ripoti ya Umoja wa Mataifa ya mwaka 2010 ilimshutumu wazi mfanyabiashara Atom kwa kuingiza silaha kutokaYemen huku akizipokea kupitia Eritrea zikiwa ni pamoja na makombora ya al-Shabab na kuwapelekea kundi hili upande wa kusini mwa Somalia.

Huku wanamgambo wa Atom wakikiri kuwa mfanyabiashara Atom amekuwa akifanikisha hayo yote kutokana na kupata fedha kutoka makampuni kadhaa ya kigeni yanayofanya biashara ya mafuta.

Serikali ya Putland kwa muda sasa imekuwa ikimtuhumu Atom kwa tabia hiyo na ushirikiano wake na kikundi cha al-Shabab kwa kusababisha mauaji ya watu wasio na hatia lakini hakuna chochote kilicholeta mabadiliko mpaka sasa.

Kundi la al-Shabab kwa sasa linawategemea mno askari wake kutoka mataifa mengi ya kigeni kama vile Iraq, Afghanstan, na Pakistan mara baada ya kujiunga na al-Qaida mapema mwanzoni mwa mwaka huu.

Maafisa wa Marekani na Uingereza kwa pamoja wanahofia kuwa vijana wa Kisomali waliopo katika mataifa haya hasa maeneo ya London na Minnesota wanapatiwa mafunzo na al-Qaida na wanaweza kurudi tena Somalia na kufanya mashambulizi mapya huku hili likiungwa mkono na Waziri Mkuu wa Somalia. Waziri Mkuu Ali akiunga mkono anasema, al-Qaida inawaajiri watoto kutoka Marekani, Uingereza na ata Somalia na kuleta mashaka ulimwenguni. Anasisitiza kuwa hawatoogopa kurudi tena Somalia.

Hammami akishiriki ugaidi kuuwawa.

Omar Hammami ambaye ni Mmarekani mzaliwa wa Alabama ni miongoni mwa wanamgambo wa al-Shabab ambapo hivi karibuni ametoa mkanda wa video unaonyesha kuhofia maisha yake baada ya yeye kutafautiana na wanamgambo wenzake.

Huku Waziri Mkuu Ali akisema bayana kuwa kwa hali hii al-Shabab na al-Qaida ni sawa na makundi mengine ya kigaidi kama vile mafia. Kiongozi huyu alipoulizwa kama serikali yao inaweza kumuua Hammami aliweka bayana kuwa kama atashiriki matukio ya kigaidi watafanya hivyo. Hammami ni miongoni mwa watu walio katika orodha ya magaidi wanaotafutwa na FBI.

Mwaka 2012 ni mwaka mwema kwa Somalia huku kukiwa na kuundwa kwa serikali ya kudumu mara baada ya utawala wa sasa kumaliza muda wake mwezi wa nane mwake huu. Huku miji kadhaa iliyokuwa ikishikiliwa na al-Shabab ikiwa chini ya Mogadishu kwa sasa, alimalizia Waziri Mkuu Ali.

Mwandishi: Adeladius Makwega/APE

Mhariri: Yusuf Saumu