1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Amri ya kijeshi yatangazwa Thailand

Ricardo von Beck20 Mei 2014

Waziri Mkuu wa mpito wa Thailand, Niwattung Boonsongpaisan leo amelitaka jeshi la taifa kufanya kazi kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo. Hii ni kauli yake ya kwanza jeshi hilo baada ya kutangaza amri ya kijeshi nchi humo

https://p.dw.com/p/1C2zH
Thailand Armee verhängt Kriegsrecht 20.05.2014
Operesheni za kijeshi zikiendelea mjini BangkokPicha: Reuters

Katika taarifa yake hiyo waziri mkuu Niwattumrong amesema kila hatua itakayofuata inapaswa kutekelezwa kwa njia ya amani, pasipo vurugu,ubaguzi na ifanyike kwa usawa pia. Aliendelea katika taarifa hiyo iliyotolewa na ofisi yake kwamba jeshi linapaswa kuzingatia katiba ya nchi hiyo.

Jeshi nchini Thailand halikushauriana na serikali katika kuweka amri ya kijeshi mjini mapema leo, katika hatua ambayo jeshi hilo imesema sio mapinduzi lakini yenye lengo la kustawisha usalama baada ya kuwepo kwa wasiwasi wa kutokea vurugu za kisiasa.

Kusuasua kwa serikali ya mpito

Niwattumrong alichukua nafasi ya Yungluck Shinawatra baada ya kuondolewa madarakani na uamuzi tata wa mahakama Mei 7. Serikali yake ambae inaongoza katika kipindi cha mpito imekuwa ikiyumba wakati waandamanaji wanaoipinga wakitafuta uungwaji mkono katika kumuondoa kiongozi huyo na kuchaguliwa mwengine.

Thailand Niwattumrong Boonsongpaisan neuer Premierminister Archiv 2013
Waziri Mkuu wa muda wa Thailand Niwattumrong BoonsonPicha: Kazuhiro Nogi/AFP/Getty Images

Wakosoaji wanasema Seneti ya Thailand inakosa mamlaka ya kuendesha hatua hiyo ya mpito. Niwattumrong anataka uchaguzi mpya, kwa lengo la kuepusha kabisa mgogoro wa taifa hilo ambao umedumu kwa takribani miezi saba sasa.

Nao wachunguzi wanasema chama tawala cha Peau, kinaonekana kama chenye uwezo wa kushinda uchaguzi mwingine wowote. Lakini waandamanaji wanaoipinga serikali wanataka mabadiliko madhubuti kabla ya uchaguzi mwingine kwa lengo la kuufikisha kikomo ushawishi wa ndugu mwenye utajili mkubwa wa Yungluck, aitwae Thaksin katika siasa za Thailand.

Ufafanuzi wa amri ya kijeshi

Katika hatua nyingine mkuu wa majeshi Thailand ameyataka makundi yanayohasimiana kuzungumza kwa pamoja na kwamba hiyo amri ya kijeshi walioiweka wataweza kuiondoa pale amani na utii wa sheria utakaporeje. Generali Prayuth Chan-ocha aliwaambia waandishi wa habari kwamba wameziomba pande zote kukaa pamoja na kuzungumza ili kufanikisha upatikanaji wa hatma njema ya taifa.

Amesema jeshi limechukua hatua hiyo kwa lengo la kuweka utii wa sheria na kujenga imani kwa wekezaji baada ya miezi kadhaa ya machafuko ya kisiasa ambayo yamevuruga uchumi wa taifa na kuongeza kuwa jeshi litachukua hatua kali dhidi ya yeyote atakaetumia silaha dhidi ya raia.

Tayari mwekezaji mkubwa nchini humo Japan ameonesha kusikitishwa kwake na kuwepo kwa amri ya kijeshi huku Marekani ikisema hatua hiyo lazima iwe ya muda na jumuiya ya kimatiafa inafuatilia kwa karibu.

Mwandishi: Sudi Mnette RTR/AFP
Mhariri:Yusuf Saumu