1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Askari wa Syria washukiwa kuchoma moto mashamba

Abdu Said Mtullya14 Juni 2011

Wakimbizi kutoka Syria wameendele kumiminikia katika miji ya mpakani nchini Uturuki kuyanusuru maisha yao kutokana na mashambulio ya wanajeshi wa serikali ya Rais Bashar al-Assad, wanaotuhumiwa pia kuchoma mashamba.

https://p.dw.com/p/11Zhl

Shirika la habari la Uturuki Anatolia limearifu kwamba watu 7000 kutoka Syria wamevuka mpaka na kuingia Uturuki ili kuyakimbia majeshi ya nchi yao yanayopambana na wapinzani wa serikali kaskazini magharibi mwa Syria.

Wakimbizi kutoka mji wa Syria wa Jisr al-Shughur, uliorejeshwa tena katika mikono ya majeshi ya nchi hiyo wamesema, wanajeshi hao wamevizingira vijiji na wamewakamata mamia ya vijana. Hatua hiyo inafuatia madai yaliyotolewa na serikali ya Syria juu ya kuuliwa maafisa wa usalama 120 na makundi ya watu waliokuwa na silaha.

Lakini wakaazi wa sehemu hiyo wamesema kuwa maafisa hao waliuliwa na majeshi ya Syria baada ya kugoma kuwashambulia waandamanaji.

Wakimbizi wanaoingia Uturuki wanesema kuwa majeshi ya Syria yanachoma moto mashamba na yanaiteketeza mifugo katika sehemu za milimani kaskazini mwa nchi. Wakimbizi hao pia wamesema kwamba baadhi ya askari wameasi ili kuwalinda raia.